Ukandamizaji dhidi ya watoto Ujerumani, zaidi ya 130 wauawa
Idara ya masuala ya jinai nchini Ujerumani imetangaza kwamba, zaidi ya watoto 130 wameuawa kutokana na ukatili wa ndani ya familia nchini humo.
Shirika la habari la IRIB limenukuu taarifa ya idara hiyo ikisema kwamba kwa mujibu wa takwimu za vitendo vya ukatili dhidi ya watoto nchini Ujerumaini za mwaka 2018, kumekuwa na ongezeko kubwa la vitendo hivyo kiasi kwamba kesi za ukatili huo dhidi ya watoto zilipindukia 14 elfu na 400 mwaka jana na watoto 136 walipoteza maisha yao kutokana na ukatili wa ndani ya familia zao.
Taarifa ya Idara ya Masuala ya Jinai ya Ujerumani imeongeza kuwa, kesi elfu nne na 129 za vitendo viovu ikiwa ni pamoja na kunajisiwa, kuwapiga watoto na kuwachoma kwa vitu moto na vyenye ncha kali ziliripotiwa mwaka huo. Wananchi wa Ujerumani wanasema kuwa, ukatili dhidi ya watoto wadogo na kutumiwa vibaya kijinsia na watu wazi ni miongoni mwa matatizo makubwa katika nchi hiyo ya Ulaya.
Ukatili na unyanyasaji wa kijinsia ni mkubwa katika nchi za Ulaya ikiwemo Ujerumani kiasi kwamba mwezi Aprili mwaka huu, shirika la habari la Reuters lilichapisha makala iliiyosema kuwa, kuna mamia ya simulizi za vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia zilizokusanywa na Taasisi Huru ya Uchunguzi ya Ujerumani.
Taasisi hiyo ilitoa ripoti ya uchunguzi wake wa miaka mitatu ikiwa na kurasa 250 zenye maelezo ya watu 1,690 waliokubali kukiri hadharani udhalilishaji huo ikiwa ni kampeni maalumu ya kuhakikisha kuwa watoto waliokumbwa na vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia hawaendelei kuteseka katika umri wao wote.