UN: Kila wiki mbili, lugha moja ya asili inapotea duniani
Uchunguzi wa Umoja wa Mataifa umebaini kuwa, kila wiki mbili, lugha moja ya asili hupotea.
Hayo yalibainika jana Agosti tisa ambayo ilikuwa siku ya kimataifa ya watu wa asili. Maadhimisho hayo yameenda sambamba na mwaka 2019 ambao ni mwaka wa kimataifa wa lugha za asili ili kulinda na kuendeleza lugha za asili.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema lugha ni jinsi ambavyo watu wanawasiliana na lugha ina uhusiano na tamaduni, historia na utambulisho.
Hata hivyo amesema licha ya umuhimu huo, nusu ya takribani lugha 6,700, idadi kubwa ikiwa ni zile za asili, ziko hatarini kutoweka. Guterres amesema, kwa kila lugha inayotoweka, dunia inapoteza utajiri wa tamaduni na ufahamu.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa hivi sasa kuna watu milioni 370 wa jamii za asili ambao Guterres amesema, “idadi kubwa wanakosa haki zao za msingi, huku mifumo iliyowekwa ya kibaguzi na uenguaji ikiendelea kutishia mbinu zao za maisha, tamaduni na utambulisho wao.”