Johnson awahutubu wabunge wa Uingereza: Niuzuluni au niacheni nitekeleze Brexit
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson amewataka wabunge wa nchi hiyo wamuuzulu au wamwache atekeleze mpango wa kujitoa nchi hiyo katika Umoja wa Ulaya, maarufu kama Brexit kwa kufikia au bila kufikia makubaliano na umoja huo.
Johnson, ambaye ameshindwa katika mpango wake wa kusimamisha vikao vya Bunge amewahutubu wabunge waliokuwa wakimzomea na kupiga makelele katika kikao cha jana akisema: Ama Bunge likae kando na kuruhusu serikali ihatimishe mchakato wa Brexit au liipigie serikali kura ya kutokuwa na imani nayo ili hatimaye liyakabili maamuzi ya wapigakura.
Bunge la Uingereza lilianza tena vikao vyake vya kawaida jana Jumatano baada ya kulazimishwa kusitisha shughuli zake kwa muda wa siku 16.
Usitishwaji huo wa vikao vya Bunge la Uingereza kwa muda wa wiki tano ulifanyika kwa ombi la Waziri Mkuu Boris Johnson na kwa idhini ya Malkia Elizabeth; hata hivyo umebatilishwa na Mahakama ya Juu Kabisa ya nchi hiyo.
Katika uamuzi iliotangaza siku ya Jumanne, mahakama hiyo ilisema, hatua ya kusimamisha vikao vya bunge ni kinyume cha sheria.
Muda mfupi kabla ya kusimamishwa, Bunge la Uingereza lilipitisha mpango unaoizuia serikali kujitoa katika Umoja wa Ulaya bila kufikia mwafaka na umoja huo.
Johnson ameahidi kuwa ifikapo tarehe 31 Oktoba, Uingereza itajitoa katika Umoja wa Ulaya iwe ni kwa maafikiano au bila kufikia mwafaka na umoja huo.../