Korea Kaskazini: Hatutosalimu amri mbele ya Marekani
Kiongozi wa Korea Kaskazini amekemea uhasama wa vikwazo na mashinikizo ya Marekani dhidi ya nchi yake na kusisitiza kwamba, kamwe serikali ya Pyongyang haitosalimu amri mbele ya Washington.
Kim Jong-un ameyasema hayo akiashiria hatua za viongozi wa Marekani ambapo ameitahadharisha pia Washington kutokana na hatua zake za uhasama dhidi ya nchi yake. Kabla ya hapo pia Ri Yong-ho, Waziri wa Mambo ya Nje wa Korea Kaskazini aliitahadharisha Marekani kuwa iwapo haitofuta vikwazo vyake dhidi ya Pyongyang basi kuna uwezekano wa nchi hiyo kuanzisha tena majaribio ya silaha za nyuklia na shughuli nyingine za kuimarisha makombora yake.
Hayo yanajiri katika hali ambayo hivi karibuni Rais Donald Trump wa Marekani alisisitizia kuendelezwa vikwazo dhidi ya nchi hiyo ya Asia maadamu hakujafikiwa maendeleo yoyote katika mazungumzo ya nchi mbili. Viongozi wakuu wa Marekani na Korea Kaskazini wamekutana mara tatu hadi sasa, ingawa bado hakujafikiwa mapatano kati yao.