Waislamu wa Norway kuwashitaki walioivunjia heshima Qur'an Tukufu
(last modified Wed, 20 Nov 2019 02:31:39 GMT )
Nov 20, 2019 02:31 UTC
  • Waislamu wa Norway kuwashitaki walioivunjia heshima Qur'an Tukufu

Viongozi wa Kiislamu nchini Norway wametangaza kwamba wamekusudia kuwasilisha mashtaka kwa jeshi la polisi la nchi hiyo kufuatia kitendo cha kuichoma moto Qur'an Tukufu kilichojiri katika mkusanyiko mmoja wa maandamano hivi karibuni.

Mtandao wa habari wa ABC Nyheter umeripoti kwamba, wanachama wa taasisi moja ya kieneo na iliyo dhidi ya Uislamu nchini humo ambayo inaitwa SIAN na ambao wamekuwa wakieneza propaganda chafu dhidi ya dini ya Kiislamu kwamba eti inaeneza ukatili, walimvunjia heshima pia Mtume wa Uislamu Muhammad (saw). Akmal Ali, mkuu wa Umoja wa Waislamu katika mji wa Agder unaoitwa 'Muslim  Union of Agder' amesema kuwa, jamii ya Waislamu nchini Norway si tu kwamba imekitaja kitendo hicho kuwa ni kinyume cha sheria, bali ni kosa ambalo limesukumwa na chuki dhidi ya dini hiyo ya mbinguni.

Waislamu wa Norway wanaokabiliwa na ubaguzi mkubwa dhidi yao

Ameashiria maandamano ya siku ya Jumapili iliyopita ya kundi linalojiita 'Zuieni Norway kuwa ya Kiislamu' na kusema kuwa, katika maandamano hayo ambayo yalifanyika katika mji wa Kristiansand, wanachama wa kundi hilo linaloupinga Uislamu walikichoma moto Kitabu Kitukufu cha Mwenyezi Mungu (Qur'an Tukufu). Kundi hilo la SIAN na lililo dhidi ya Uislamu liliasisiwa mwaka 2000 ambapo lengo lake ni kukabiliana na ongezeko la wafuasi wa dini hiyo nchini Norway. Aidha kundi hilo linadai kwamba, dini ya Uislamu inakiuka katiba ya nchi hiyo kama ambavyo eti inakinzana na matukufu ya kidemokrasia na ubinaadamu.