Ujerumani yaunga mkono hatua kali za Poland dhidi ya wahajiri
Akizungumza na Waziri Mkuu wa Poland katika ziara yake nchini humo, Kansela mpya wa Ujerumani amesema kuwa Poland imewajibika kwa maslahi ya Ulaya.
Olaf Scholz jana usiku alielekea huko Poland baada ya kuzitembele Paris na Brussels na kukutana huko Warsaw na Mateusz Morawiecki, Waziri Mkuu wa Poland. Kansela mpya wa Ujerumani ameunga mkono hatua kali za Poland dhidi ya wahajiri na kueleza kuwa, katika hilo, Poland imefanya kazi kwa maslahi ya Ulaya na kwamba yuko pamoja na nchi hiyo.
Wakati huo huo Waziri Mkuu wa Poland ameendelea kuituhumu serikali ya Belarus na kudai kuwa nchi hiyo inawatumia binadamu kama silaha na ngao ya kujilinda.
Nchi za Magharibi zinaituhumu Belarus kuwa ndiyo iliyosababisha mgogoro wa wahajiri kwa kuwarubuni wahamiaji kuelekea katika maeneo ya mpakani kwa ahadi nyepesi; jambo ambalo linahesabiwa kama hatua ya Minsk ya kulipiza kisasi kufuatia vikwazo vya Umoja wa Ulaya dhidi ya Belarus. Wiki iliyopita Umoja wa Ulaya uliiwekea vikwazo vipya Belarus kutokana na mgogoro wa wahajiri.