Ijumaa, tarehe Mosi, Disemba 2023
Leo ni Ijumaa tarehe 17 Jumadil Awwal 1445 Hijria sawa na Tarehe Mosi Disemba 2023.
Siku kama ya leo miaka 1154 iliyopita, alifariki dunia Abul-Abbas Ahmad Ibn Yahya Tha’lab, msomi mashuhuri wa lugha na nahau. Tha’labi aliyekuwa na asili ya Iran ya alizaliwa mwaka 200 Hijiria mjini Baghdad. Kutokana na kumbukumbu yake nzuri alijifunza kwa haraka elimu ya nahau, lugha ya Kiarabu, kusoma Qur’ani na hadithi mbele ya walimu wa zama hizo. Akiwa kijana mdogo tayari alikuwa amehifadhi fasihi ya lugha ya Kiarabu ambapo alilipa umuhimu suala hilo huku akifikia daraja ya juu katika uga huo. Miongoni mwa athari zilizosalia hii leo kutoka kwa Abul-Abbas Ahmad Ibn Yahya Tha’lab ni kitabu cha ‘Majaalisu Tha’lab’ ‘Kitabul-Faswiih’ na ‘Qawaidu al-Shi’r.’

Miaka 995 iliyopita katika siku kama hii ya leo alizaliwa mmoja wa wasomi na wanafalsafa wakubwa wa Kiislamu na Kiirani, Abu Hamid Muhammad Ghazali, maarufu kwa jina la Imam Muhammad Ghazali. Ghazali alisoma elimu ya fiq'hi kutoka kwa Abu Nasri Ismail na baada ya kufikia umri wa miaka 28 alikuwa mmoja wa wasomi wakubwa wa Kiislamu katika elimu hiyo. Umaarufu wa Imam Muhammad Ghazali ulipelekea kiongozi wa Iraq wakati huo Khoja Nidham al-Mulk kumwalika msomi huyo kwenda mjini Baghdad kwa ajili ya kufundisha. Hatimaye alirejea Iran na kujishughulisha na masuala ya ualimu. Kabla ya kurejea Iran, Imam Muhammad Ghazali alipata kuandika vitabu vya thamani kama "Ihyau Ulumuddin," "Kemia ya Saada" na "Nasaha za Wafalme".
Katika siku kama ya leo miaka 198 iliyopita, muungano wa kihistoria wa nchi za Ulaya uliojulikana kama Muungano Mtakatifu ulisambaratika baada ya kujiengua utawala wa Kikaitsar (Tsarist) wa Russia katika muungano huo. Baada ya kuanguka kwa utawala wa Napoleon, muungano huo ukaunda Congress ya Vienna, kati ya tawala za Russia, Austria na ufalme wa Pros na serikali hizo zikaafikiana kwamba nchi zilizo chini ya utawala wa muungano huo na katika uhusiano wa kimataifa zifuate misingi ya dini ya Kikristo.
Siku kama hii ya leo miaka 85 iliyopita Ayatullah Sayyid Hassan Mudarres, mwanazuoni mwanamapambano na mpigania ukombozi wa Kiirani aliuawa shahidi na vibaraka wa Reza Khan, mtawala dhalimu wa Iran wa wakati huo katika mji wa Kashmar kaskazini mashariki mwa Iran. Ayatullah Sayyid Hassan Mudarres aliamua kuanzisha mapambano dhidi ya utawala huo baada ya kujionea dhulma na ukandamizaji wa mtawala Reza Khan nchini Iran. Alifanya jitihada kubwa za kutekelezwa sheria za Kiislamu hapa nchini na kuiokoa Iran kutoka kwenye makucha na udhibiti wa wakoloni. Kwa msingi huo mtawala kibaraka wa wakati huo wa Iran, Reza Khan Pahlavi alimuona kuwa adui mkubwa na kuchukua uamuzi wa kumuua.
Siku kama ya leo miaka 50 iliyopita David Ben-Gurion mmoja wa waasisi wa utawala wa Kizayuni wa Israel na Waziri Mkuu wa kwanza wa utawala huo ghasibu aliaga dunia akiwa na umri wa miaka 87. Ben-Gurion alizaliwa tarehe 16 Oktoba 1886 katika mji wa Plonsk huko Uholanzi ambayo katika zama hizo ilikuwa sehemu ya ardhi ya ufalme wa Russia. Alielekea katika ardhi za Palestina mwaka 1906 akiwa na umri wa miaka 20 na kuasisisi harakati ya Kiyahudi. Katika Vita vya Kwanza vya Dunia David Ben-Gurion alikuwa na nafasi kubwa katika kuwahamisha taratibu Mayahudi kwenda ardhi za Palestina. Katika kipindi cha Vita vya Pili vya Dunia harakati hiyo ilishika kasi chini ya uungaji mkono wa madola makubwa hususan Uingereza, kiasi kwamba mwaka 1948 sawa na tarehe 5 Mei na baada ya kupitishwa azimio na Umoja wa Mataifa la kuigawa Palestina katika pande mbili za Kiyahudi na Palestina, kulitangazwa rasmi kuanzishwa utawala haramu wa Kizayuni na wa kibaguzi wa Israel. Masaa machache baadaye, Marekani na Urusi ya zamani zikatangaza kuutambua utawala huo khabithi.
Na tarehe Mosi Disemba kila mwaka, nchi mbalimbali duniani huadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Ukimwi. Ukimwi ni ugonjwa wa kuambukiza ambao unatokana na kurundikana kwa virusi vya HIV mwilini ambavyo huharibu mfumo wa ulinzi wa mwili na kutayarisha mazingira ya kushambuliwa na maradhi nyemelezi. Ugonjwa huu ulibainika kwa mara ya kwanza kabisa nchini Marekani mwazoni mwa miaka ya 1980. Wakati huo baadhi ya wanaume wanaofanya ngono kinyume na maumbile huko New York na California waligundulika kuwa na kansa ambazo hazikukubali tiba ya aina yoyote. Japokuwa wakati huo, haikujulikana sababu ya maambukizi ya ghafla ya magonjwa hayo lakini tukio hilo limetambuliwa kuwa ndiyo mwanzo wa kujitokeza maradhi ya Ukimwi. Ugonjwa huo ambao haukuwa na jina ulienea kwa kasi kubwa katika kipindi cha mwaka mmoja na hatimaye mwaka 1982 ulipewa jina la Ukimwi.
