Dec 09, 2023 23:12 UTC
  • Jumapili, 10 Disemba, 2023

Leo ni Jumapili tarehe 26 Mfunguo Nane Jamadul-Awwal 1445 Hijria mwafaka na tarehe 10 Disemba 2023 Miladia.

Siku kama ya leo miaka 1165 iliyopita, sawa na tarehe 26 Jamadil Awwal 1437 Hijria, alifariki dunia Ibn Tayfur, mwandishi na malenga wa Kiarabu. Ibn Tayfur alizaliwa mwaka 204 Hijiria. Baada ya kuhitimu masomo yake ya awali, alijishughulisha na uandishi wa vitabu mjini Baghdad. Katika kipindi hicho Ibn Tayfur alifahamiana na maulama na wasomi mashuhuri wa mji wa Baghdad. Ni baada ya hapo ndipo Ibn Tayfur akawa mashuhuri katika uwanja wa mashairi. Mbali na uwanja huo, msomi huyo alijulikana sana kwa uandishi wa vitabu mbalimbali ambavyo hii leo vinapatikana katika maktaba za mji wa Baghdad, Iraq. ***

Siku kama ya leo miaka 193 iliyopita, alizaliwa Bi Emily Dickinson malenga wa Kimarekani. Bi Emily alijiendeleza na masomo yake katika ngazi ya Chuo Kikuu nchini Marekani. Aidha alivutiwa na fasihi ya lugha na kutunga mashairi baada ya kufahamiana na baadhi ya waandishi mashuhuri wa Kimarekani. Malenga huyo wa Kimarekani aliweza kutunga beti karibu elfu mbili za mashairi, ambapo sehemu tatu tu za mashairi hayo zilichapishwa wakati wa uhai wake na zilizosalia zikachapishwa baada ya kuaga kwake dunia. ***

Bi Emily Dickinson

 

Miaka 127 iliyopita katika siku kama hii ya leo alifariki dunia mwanakemia maarufu wa Sweden, Alfred Bernhard Nobel. Nobel alizaliwa mwaka 1833 na kuhamia nchini Russia wakati wa ujana wake. Alfred Nobel alifanikiwa kuvumbua dynamite au baruti baada ya kufanya utafiti mkubwa kwa miaka kadhaa katika uwanja wa sayansi ya kemia. Hata hivyo mada hiyo badala ya kutumiwa kwa matumizi ya amani, ilianza kutumiwa kama kifaa cha kivita. Ni kwa sababu hiyo, ndipo Nobel akatoa pendekezo la kutolewa tuzo kila mwaka kwa shakhsia aliyefanya juhudi kubwa katika uwanja wa kuimarisha amani na usalama duniani. Tuzo hiyo ambayo imepewa jina la mwasisi wake yaani Nobel mwenyewe, hutolewa katika nyanja tano za fizikia, kemia, tiba, fasihi na amani ya kimataifa kwa wasomi waliofanya jitihada kubwa za kuleta amani na mafanikio ya kielimu, uvumbuzi, na mambo mengine makubwa duniani. Hata hivyo uteuzi wa washindi wa tuzo ya Nobel hususan ile ya amani duniani umeathiriwa na ushawishi wa baadhi ya madola makubwa na kuiondoa tuzo hiyo katika mkondo wa asili wa mwanzilishi wake. ***

Alfred Bernhard Nobel

Katika siku kama hii ya leo miaka 75 iliyopita, yaani tarehe 10 mwezi Disemba mwaka 1948, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipasisha Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu na kuidhinisha haki za kimsingi na kijamii za binadamu. Azimio hilo la haki za binadamu lilitayarishwa kwa maelekezo ya Umoja wa Mataifa kupitia jopo la wawakilishi wa nchi kadhaa duniani. Kipengee nambari moja cha azimio hilo kinasisitiza kuwa binadamu wote ni sawa. Licha ya kupasishwa azimio hilo, leo hii vitendo na siasa za madola ya Magharibi hasa Marekani vinakinzana wazi na azimio hilo. Leo hii pia baadhi ya madola hayo ya Magharibi yamekuwa yakilitumia suala la haki za binaadamu kama wenzo wa kuyashinikiza mataifa mengine. ***