Alkhamisi, tarehe 16 Mei, 2024
Leo ni Alkhamisi tarehe 7 Dhilqaada 1445 Hijria sawa na tarehe 16 Mei mwaka 2024.
Miaka 729 iliyopita katika siku kama ya leo alifariki dunia Ibn Baswis mtaalamu wa kaligrafia maarufu kwa jina la Damashqi.
Alizaliwa mwaka 651 Hijiria katika mji wa Damascus na kwa muda wa miaka 50 alijishughulisha kufundisha hati na wakaazi wa mji huo walistafidi kwa elimu na sanaa kutoka kwake.
Ibn Baswis aliandika hati kwa mitindo tofauti ya kupendeza na katika umri wake wa uzeeni aliandika nakala ya Qur'ani Tukufu kwa kutumia maji ya dhahabu na kwa hati nzuri na za kuvutia. Qur'ani hiyo pamoja na athari nyingine za Ibn Basis bado ziko hadi leo. ****

Siku kama ya leo miaka 522 iliyopita, ardhi ya Honduras inayopatikana leo huko Amerika Kusini iliunganishwa na makoloni ya Muhispania.
Kabla ya hapo Honduras ilikuwa kituo cha utamaduni wa kaumu ya Maya. Hata hivyo baada ya Honduras kuvamiwa na kukaliwa kwa mabavu na Uhispania, kabila hilo liliangamizwa na kupotea.
Mwanzoni mwa karne ya 19 Miladia na kutokana na kuvurugika hali ya ndani ya Uhispania, Honduras kama ilivyokuwa kwa makoloni mengine, ilitumia fursa hiyo kuweza kujipatia uhuru wake. ****

Tarehe 16 Mei miaka 236 iliyopita alizaliwa mjini Hamburg, Friedrich Ruckert, malenga na mtaalamu wa masuala ya Mashariki wa Ujerumani.
Alifanya juhudi ya kutafsiri mashairi ya lugha za Kifarsi, Kiarabu na Kichina kwa lugha ya Kijerumani. Kadhalika alijifunza fasihi na tamaduni za Mashariki mwa dunia na kuzitumia katika utunzi wa mashairi.
Friedrich Ruckert alikuwa mmoja wa malenga wa Kijerumani waliofasiri diwani ya mashairi ya Hafez (malenga mkubwa wa Kiirani) katika lugha ya Kijerumani. Miongoni mwa athari ya Friedrich Ruckert ni kitabu cha 'Spring of Love.'
Katika siku kama hii ya leo miaka 108 iliyopita Ufaransa na Uingereza ziligawana makoloni yao katika Mashariki ya Kati na maeneo yaliyokuwa yakidhibitiwa na utawala wa Dola ya Othmaniyya chini ya mkataba wa Sykes-Picot, ambao ulikuwa umetiwa saini wiki moja kabla.
Kutiwa saini kwa mkataba wa kikoloni wa Sykes-Picot Agreement baada ya Vita vya Kwanza vya Dunia kulitayarisha mazingira ya kisiasa ya kugawanywa ardhi ya Mashariki ya Kati na kusambaratisha dola la Othmaniyya. Kwa mujibu wa makubaliano hayo, nchi za Uingereza na Ufaransa ziligawana udhibiti wa nchi za Kiarabu ambazo zilizokuwa chini ya dola ya Othmaniyya.
Kwa utaratibu huo, Iraq na Jordan ziliwekwa chini ya udhibiti wa Uingereza, Syria na Lebanon zikawa chini ya mamlaka ya Ufaransa. Maeneo ya kaskazini mwa Iraq na mashariki mwa Uturuki pia yalikabidhiwa kwa Urusi. Miongoni mwa matokeo mabaya sana ya makubaliano Sykes-Picot ni kuundwa kwa utawala wa kibaguzi wa Israel katika ardhi ya Palestina, jambo ambalo lilifanyika takriban miongo mitatu baada ya kutiwa saini makubaliano hayo.

Miaka 37 iliyopita katika siku kama ya leo, wakati wa vita vya kulazimishwa vya majeshi ya Iraq dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, ndege za kivita za Iraq ziliishambulia manowari ya kivita ya Marekani iitwayo Stark katika eneo la Ghuba ya Uajemi, na kupelekea wanajeshi 37 wa Kimarekani kuuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Baada ya tukio hilo, utawala wa Saddam uliomba radhi kwa serikali ya Marekani na kutangaza kuwa tayari kulipa fidia za uharibifu huo.

Siku kama ya leo miaka 36 iliyopita, Jeshi Jekundu la Umoja wa Kisovieti lilianza kuondoka nchini Afghanistan.
Baada ya Nur Muhammad Taraki kupinduliwa, serikali ya kwanza ya kikomunsti iliyokuwa ikipata himaya ya moja kwa moja ya Urusi ya zamani ilianzishwa nchini Afghanistan. Utawala wa Taraki uliondolewa madarakani mwanzoni mwa mwaka 1979 kupitia mapinduzi mengine yaliyoongozwa na Hafidhullah Amin mmoja wa watu wake wa karibu.
Lakini Warusi hawakumpenda Hafidhullah ambaye alikuwa akitaka kujikurubisha kwa Marekani na kuanzisha uhusiano kati ya Afghanistan na Mashariki na vilevile Magharibi na hivyo wakaipindua serikali yake. ***
Siku kama ya leo miaka 27 iliyopita, Jenerali Mobutu Sese Seko rais na dikteta wa zamani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Zaire ya zamani, aliikimbia nchi hiyo baada ya vikosi vya majeshi ya waasi vilivyokuwa vikiongozwa na Laurent Kabila kukaribia mji wa Kinshasa.
Mobutu alichukua madaraka ya nchi hiyo mnamo mwaka 1965 kupitia mapinduzi ya kijeshi na kisha kutawala kwa muda wa miaka 32. Licha ya kiongozi huyo kuwa dikteta asiye na huruma, lakini alikuwa akiungwa mkono na madola ya Magharibi hasa Marekani na Ufaransa.
Kutokana na Congo DR kuwa katika eneo nyeti na muhimu kijiografia katikati mwa bara la Afrika na kuwa na utajiri mkubwa wa madini ikiwemo almasi, imekuwa ikizingatiwa sana na kumezewa mate na nchi za Magharibi. Siku moja baada ya Mobutu kuikimbia nchi hiyo, vikosi vya waasi viliuteka mji wa Kinshasa na kiongozi wao yaani Laurent Kabila, akashika hatamu za uongozi wa nchi.
Siku kama ya leo miaka 15 iliyopita, alifariki dunia Ayatuhil Udhma Muhammad Taqi Behjat Foumani, mmoja wa Marajii Taqlidi na maurafaa wakubwa wa Kiislamu.
Alizaliwa mwaka 1294 Hijria Shamsia katika mji wa Fouman ulioko katika mkoa wa Gilan kaskazini mwa Iran. Baada ya kupata elimu ya msingi ya kidini, mwaka 1308 Hijria Shamsia alielekea katika Chuo Kikuu cha Kidini cha Najaf nchini Iraq.
Ayatullah Bahjat alikuwa mashuhuri sana kutokana na uchamungu wake. Kitabus Swalat, Jamiul Masail na Wasilatun Najat ni baadhi ya vitabu mashuhuri vya msomi huyo.