Jumatatu tarehe 27 Novemba, 2017
Leo ni Jumatatu tarehe 8 Rabiul Awwal 1439 Hijria sawa na 27 Novemba 2017.
Miaka 1179 iliyopita, inayosadifiana na tarehe 8 Rabiul Awwal 260 Hijria, aliuawa shahidi Imam Hassan al Askari (AS) mmoja kati ya Watu wa Nyumba ya Mtume Mtukufu SAW katika mji wa Samarra nchini Iraq. Imam Askari AS alizaliwa mwaka 232 Hijria katika mji wa Madina na alichukua jukumu la kuongoza Umma wa Kiislamu baada ya kuuawa shahidi baba yake, Imam Hadi (AS). Kipindi cha Uimamu wake kilikuwa kigumu na nyeti sana kutokana na kuzaliwa Imam wa Zama Mahdi (AS) wakati huo. Alichukua hatua kubwa za kuhuisha Uislamu na kueneza maarifa sahihi na asili ya dini hiyo ya Mwenyezi Mungu. Imam Hassan al Askari aliuawa shahidi kwa kupewa sumu na utawala wa Bani Abbas.

Siku kama ya leo miaka 316 iliyopita, sawa na tarehe 27 Novemba mwaka 1701, Anders Celsius mwanafizikia na mtafiti wa Sweden alizaliwa katika mji wa Uppsala, uliokuwa makao makuu ya utamaduni ya nchi hiyo. Familia yake ilikuwa ya wasomi na baba na babu yake walikuwa wanahisabati. Celsius alivutiwa sana na elimu ya nujumu na mwaka 1730 alifanikiwa kuwa mwalimu wa nujumu katika chuo kikuu cha Uppsala. Mwaka 1742 alipendekeza kutumika daraja ya kipima joto kwa mujibu wa Celsius, iliyoitwa kwa jina lake. Mpangilio huo ulikubaliwa rasmi na kuanza kutumika duniani mwaka 1945, ikiwa ni mwaka mmoja baada ya kufariki dunia mwanafizikia huyo.
Tarehe 27 Novemba miaka 98 iliyopita iliainishwa mipaka mipya ya nchi za Ulaya na Mashariki ya Kati baada ya kumalizika Vita vya Kwanza vya Dunia. Baada ya kumalizika vita hivyo na kutiwa saini mkataba wa amani wa Versay, kulisainiwa mikataba mingine kadhaa ya kuainisha mustakbali wa tawala za Austria na Hungari na utawala wa Othmania na nchi ya Bulgaria ambayo kila mmoja ulikuwa na masharti mazito na kutoa fidia nchi hizo kwa zile zilizopata ushindi. Kuainishwa kwa mipaka mipya ya nchi za Ulaya na Mashariki ya Kati katika mkutano wa Paris kulibadili kabisa ramani ya dunia.
Na siku kama ya leo miaka 74 iliyopita, mkutano wa siku 3 wa viongozi wa Marekani, Uingereza na Umoja wa Sovieti ulifanyika mjini Tehran katika hali ambayo, Iran wakati huo ilikuwa chini ya udhibiti wa majeshi ya nchi hizo. Mkutano wa Tehran ulifanyika baada ya Marekani kuingia katika Vita vya Pili vya Dunia na kuzuka kambi mpya dhidi ya majeshi ya Ujerumani. Walioshiriki katika mkutano huo walikuwa Rais Franklin Delano Roosevelt wa Marekani, Waziri Mkuu wa Uingereza, Winston Churchill na Joseph Stalin kiongozi wa wakati huo wa Umoja wa Kisovieti.