Nov 26, 2019 22:14 UTC
  • Jumatano tarehe 27 Novemba 2019

Leo ni Jumatano tarehe 29 Rabiul Awwal 1441 Hijria sawa na tarehe 27 Novemba 2019.

Siku kama ya leo miaka 318 iliyopita, sawa na tarehe 27 Novemba mwaka 1701, Anders Celsius mwanafizikia na mtafiti wa Sweden alizaliwa katika mji wa Uppsala, uliokuwa makao makuu ya utamaduni ya nchi hiyo. Familia yake ilikuwa ya wasomi na baba na babu yake walikuwa wanahisabati. Celsius alivutiwa sana na elimu ya nujumu na mwaka 1730 alifanikiwa kuwa mwalimu wa nujumu katika chuo kikuu cha Uppsala. Mwaka 1742 alipendekeza kutumika daraja ya kipima joto kwa mujibu wa Celsius, iliyoitwa kwa jina lake. Mpangilio huo ulikubaliwa rasmi na kuanza kutumika duniani mwaka 1945, ikiwa ni mwaka mmoja baada ya kufariki dunia mwanafizikia huyo.

Anders Celsius

Tarehe 27 Novemba miaka 100 iliyopita iliainishwa mipaka mipya ya nchi za Ulaya na Mashariki ya Kati baada ya kumalizika Vita vya Kwanza vya Dunia. Baada ya kumalizika vita hivyo na kutiwa saini mkataba wa amani wa Versay, kulisainiwa mikataba mingine kadhaa ya kuainisha mustakbali wa tawala za Austria, Hungary, utawala wa Othmania na nchi ya Bulgaria ambayo kila mmoja ulikuwa na masharti mazito na kutoa fidia nchi hizo kwa zile zilizopata ushindi. Kuainishwa kwa mipaka mipya ya nchi za Ulaya na Mashariki ya Kati katika mkutano wa Paris kulibadili kabisa ramani ya dunia.

Utawala wa Othmania kabla ya kugawanywa

Na siku kama ya leo miaka 76 iliyopita, mkutano wa siku 3 wa viongozi wa Marekani, Uingereza na Umoja wa Sovieti ulifanyika mjini Tehran katika hali ambayo, Iran wakati huo ilikuwa chini ya udhibiti wa majeshi ya nchi hizo. Mkutano wa Tehran ulifanyika baada ya Marekani kuingia katika Vita vya Pili vya Dunia na kuzuka kambi mpya dhidi ya majeshi ya Ujerumani. Walioshiriki katika mkutano huo walikuwa Rais Franklin Delano Roosevelt wa Marekani, Waziri Mkuu wa Uingereza, Winston Churchill na Joseph Stalin kiongozi wa wakati huo wa Umoja wa Kisovieti.

Rais Franklin Delano Roosevelt wa Marekani, Waziri Mkuu wa Uingereza, Winston Churchill na Joseph Stalin