Ijumaa tarehe 29 Novemba 2019
Leo ni Ijumaa tarehe Pili Rabiuthani 1441 Hijria sawa na Novemba 29 mwaka 2019.
Siku kama ya leo 499 iliyopita, Ferdinand Magellan baharia wa Kihispania alifanikiwa kuvuka mkono bahari ambao leo hii umepewa jina lake yaani Lango Bahari la Magellan na akafika katika bahari ya Pacific kupitia bahari ya Atlantic. Wakati huo Ferdinand Magellan alikuwa akijishughulisha na masuala ya uvumbuzi wa baharini katika pwani ya Amerika ya Kusini.
Miaka 76 iliyopita sawa na tarehe 29 Novemba 1943 harakati ya Ukombozi ya kupambana na ufashisti iliundwa nchini Yugoslavia chini ya uongozi wa Marshal Tito. Wapiganaji wa harakati hiyo walitoa pigo kubwa kwa wanajeshi wa Ujerumani wakati Yugoslavia ilipokuwa ikikaliwa kwa mabavu na jeshi la Ujerumani. Mwaka 1944 wapiganaji wa harakati ya kupambana na ufashisti nchini Yugoslavia waliwafukuza nchini mwao wanajeshi vamizi wa Ujerumani kwa kusaidiwa na Jeshi Jekundu la Urusi ya zamani.
Siku kama ya leo miaka 72 iliyopita mwafaka na tarehe 29 Novemba 1947, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipasisha kwa wingi dhaifu wa kura suala la kugawanywa ardhi za Palestina baina ya serikali mbili yaani ya Palestina na ya Kiyahudi. Uamuzi huo usio wa kiadilifu na usio wa kimantiki ulichukuliwa chini ya ushawishi wa serikali za Magharibi hususan Marekani na Uingereza.

Miaka 25 iliyopita katika siku kama ya leo, inayosadifiana na tarehe 8 Azar mwaka 1373 alifariki dunia Ayatullah Muhammad Ali Araki, mmoja wa marjaa wakubwa wa taqlidi wa Waislamu akiwa na umri wa miaka 103. Mwanzuoni huyo wa Kiislamu alizaliwa katika mji wa Arak katikati mwa Iran na tangu akiwa na umri mdogo alikuwa na shauku kubwa ya kujifunza elimu ya dini. Ayatullah Muhammad Ali Araki kwa muda mrefu alifundisha katika chuo kikuu cha kidini cha Qum na miongoni mwa vitabu vyake ni risala ya Ijitihadi na Taqlidi pamoja na Sherhe ya Uruwatul Uthqaa.
Na miaka 9 iliopita sawa na tarehe 8 mwezi Azar mwaka 1389 Hijria Shamsia, Madakta Majid Shahriyari na Fereydun Abbasi waliokuwa Wahadhiri wa Fizikia ya Nyuklia wa Iran walilengwa katika mashambulio mawili tofauti ya kigaidi mjini Tehran. Dakta Abbasi alijeruhiwa ambapo Dakta Majid Shahriyari Mhadhiri wa Chuo Kikuu, Mwanafizikia na Msomi wa Nyuklia wa Iran akauawa shahidi katika shambulio hilo. Magaidi waliofanya jinai hiyo walitiwa nguvuni na kukiri kwamba wanashirikiana na shirika la ujasusi la Israel MOSSAD.