May 02, 2023 01:20 UTC
  • Jumanne tarehe Pili Mei 2023

Leo ni Jumanne tarehe 11 Shawwal 1444 Hijria sawa na tarehe Pili Mei 2023.

Tarehe 11 Shawwal miaka 1447 iliyopita Mtume Muhammad (S.A.W) alielekea katika mji wa Twaif karibu na Makka kwa lengo la kuwalingania Uislamu watu wa kabila la Thaqif. Safari hiyo ya Mtume mtukufu ilifanyika katika kipindi ambacho alikuwa ameondokewa na ami na mlezi wake kipenzi, Abu Twalib, jambo lililowafanya Maquraish wa Makka wazidishe maudhi na manyanyaso dhidi ya Mtume Muhammad (S.A.W) na wafuasi wake. Hivyo ilitarajiwa kuwa, iwapo wakazi wa Twaif wangekubali Uislamu, mji huo ungeweza kuwa kituo na makazi salama kwa Waislamu waliokuwa wakidhulumiwa wa Makka. Hata hivyo viongozi wa kabila la Thaqif sio tu kwamba hawakumwamini Mwenyezi Mungu Mmoja na risala ya Mtume Muhammad (S.A.W), bali pia baadhi ya watu wa kabila hilo walimfanyia maudhi, dhihaka na kumjeruhi Mtume Muhammad (saw).

Twaif

Katika siku kama ya leo miaka 504 iliyopita, alifariki dunia mchoraji na msanifu majengo maarufu wa Italia, Leonardo da Vinci. Alizaliwa mwaka 1452 na umahiri wake ulidhihiri haraka katika nyanja mbalimbali za sanaa. Baada ya kufanya safari katika miji kadhaa ya Italia, mwaka 1506 Da Vinci alielekea Ufaransa na kuwa mchoraji wa Mfalme Louis xii (12). Aliishi katika kipindi cha mchoraji mwingine mashuhuri wa Italia, Michelangelo, na wasanii hao wawili mashuhuri walitoa mchango mkubwa katika sanaa ya kipindi cha mwamko wa Ulaya (Renaissance). Miongoni mwa michoro maarufu ya Leonardo Da Vinci ni The "Last Supper" na "Mona Lisa".  Mbali na uchoraji, Leonardo Da Vinci alibobea pia katika taaluma nyingine kama hisabati.

Leonardo Da Vinci

Miaka 66 iliyopita katika siku kama hii ya leo alifariki dunia Seneta wa chama cha Republican huko Marekani Joseph McCarthy. Katika kipindi cha vita baridi McCarthy alikuwa kiongozi wa moja ya kamati za Baraza la Seneti la Marekani. Mwanasiasa huyo aliwasilisha orodha ya majina ya wafanyakazi 205 wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani akidai kwamba wanafanya ujasusi kwa maslahi ya Urusi ya zamani. Hatua hiyo ilikuwa mwanzo wa harakati iliyopewa jina la McCarthyism ambayo kwa mujibu wake wasomi, wasanii na maafisa wengi serikalini walifuatiliwa na kuswekwa jela kwa kutuhumiwa kwamba wanafanya ujasusi kwa maslahi ya Urusi na kwamba wana fikra za kikomunisti. Tume ya McCarthy ilifukuza maelfu ya wafanyakazi wa serikali na kuwasweka jela wasanii na waandishi wengi kwa tuhuma zisizo na msingi wowote. Miongoni mwa wasanii mashuhuri walioswekwa jela na tume hiyo ni Charlie Chaplin na Alfred Hitchcock.

Miaka 44 iliyopita katika siku kama ya leo, mwafaka na tarehe 12 Ordibehesht 1358 Hijria Shamsia, mwanachuoni na mwanafikra mashuhuri wa Kiislamu, Ayatullah Murtadha Mutahhari, aliuawa shahidi na kundi lililokuwa dhidi ya Mapinduzi la Furqan hapa nchini. Tukio hilo lilitokea katika kipindi cha chini ya miezi mitatu baada ya kupata ushindi Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran. Shahidi Mutahhari alijistawisha kielimu kutoka kwa maulamaa wakubwa wakiwemo Ayatullahil Udhma Burujerdi, Allamah Tabatabai na Imam Ruhullah Khomeini MA, mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Ayatullah Murtadha Mutahhari ameandika makumi ya vitabu katika taaluma mbalimbali.

Ayatullah Murtadha Mutahhari

Katika siku kama ya leo miaka 12 iliyopita Usama bin Laden kiongozi wa kundi la kigaidi la al-Qaeda aliuawa na vikosi vya Marekani huko nchini Pakistan. Usama aliyekuwa mmoja wa waasisi wa al-Qaeda alizaliwa Machi mwaka 1957 huko Riyadh nchini Saudi Arabia na kusoma katika Chuo Kikuu cha King Abdul-Aziz. Kundi la kigaidi la al-Qead linahusishwa na mauaji mengi duniani likiweko shambulio ya Septemba 11 mwaka 2001 na mashambulio ya mabomu dhidi ya balozi za Marekani Dar es Salaam Tanzania na Nairobi Kenya.