Indonesia: Tupo tayari kuendelea kuwekeza Tanzania
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Stanslaus Nyongo amesema kuwa, Jamhuri ya Indonesia itaendelea kuwekeza nchini Tanzania katika sekta mbalimbali.
Nyongo amebainisha hayo alipokutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Indonesia, Pahala Mansury ambaye amefanya safari nchini Tanzania kwa ajili ya kuikaribisha Tanzania kwenye Kongamano la Biashara kati ya Indonesia na nchi za Afrika (Indonesia – Africa Forum).
“Ujumbe wa Jamhuri ya Indonesia, ukiongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje umefika hapa kwa ajili ya kutualika kwenye Kongamano la Biashara litakalofanyika kuanzia Septemba 1-3, 2024 nchini Indonesia, sisi tumekubali kushiriki Kongamano hilo,” amesema Naibu Wzairi huyo wa nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji wa Tanzania.
Aidha amesema,wamejadiliana masuala mbalimbali ikiwemo nchi hiyo ya Indonesia kwenda kuwekeza Tanzania kwenye sekta za uzalishaji wa Kilimo, uzalishaji wa nishati safi, pamoja na uwekezaji kwenye masuala mitandao mbalimbali, Viwanda na Miundombinu.