WFP inasaka dola milioni 200 za kuongeza misaada ya kibinadamu Somalia
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i114414-wfp_inasaka_dola_milioni_200_za_kuongeza_misaada_ya_kibinadamu_somalia
Mpango wa Chakula Duniani (WFP) ulisema jana Jumanne kwamba unahitaji dola milioni 199.8 za kuweza kuongeza shughuli zake za kibinadamu kote Somalia kwa muda wa miezi sita ijayo.
(last modified 2024-07-24T02:56:36+00:00 )
Jul 24, 2024 02:56 UTC
  • WFP inasaka dola milioni 200 za kuongeza misaada ya kibinadamu Somalia

Mpango wa Chakula Duniani (WFP) ulisema jana Jumanne kwamba unahitaji dola milioni 199.8 za kuweza kuongeza shughuli zake za kibinadamu kote Somalia kwa muda wa miezi sita ijayo.

Shirika hilo limesema kuwa, idadi ya watu wasio na chakula nchini Somalia imepungua sana, na hilo linatokana na kunyesha mvuta za kutosha na kutolewa misaada endelevu ya kibinadamu.

Pamoja na hayo ripoti ya karibuni kabisa ya shirika hilo imesema kuwa, licha ya hali kuboreka, lakini athari zinazoendelea za ukame wa kihistoria, migogoro, ukosefu wa usalama, changamoto za uchumi na mafuriko makubwa yanayosababishwa na El Nino ni mambo ambayo yanaendelea kuathiri sana jamii zilizoko hatarini nchini Somalia.

Vita vya ndani na majanga mengine vimeiweka Somalia katika hali ngumu sana.

 

Shirika hilo la Umoja wa Mataifa pia limesema kuwa, mwezi uliopita wa Juni liliwafikishia misaada watu milioni 3, huku msaada wa dola milioni 12.7 ukiwa umetolewa kupitia fedha taslimu.

Pia limesema, Wasomali takriban milioni 6.9 wanakadiriwa kuhitaji msaada mwaka 2024, huku watu milioni 3.4 wakitarajiwa kukabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula mwezi huu.

Taarifa hiyo ya WFP pia imesema kuwa, msimu wa mvua wa Gu uliomalizika hivi karibuni ambao huja baina ya Aprili hadi Juni ulikuwa na mvua kubwa zaidi na mafuriko yaliyowaathiri watu 268,000 na kusababisha watu 81,000 kuhama maeneo yao kutokana na rasilimali zao za maisha kuharibiwa na mvua hizo.

Kwa mujibu wa WFP, utabiri wa awali wa hali ya hewa unaonyesha kuwa ukame na mvua zinazoweza kunyesha chini ya wastani katika msimu ujao wa mvua zitaendelea nchini Somalia.