Walibya 95 wakamatwa Afrika Kusini katika kambi ya kijeshi inayoshukiwa
Polisi nchini Afrika Kusini imetangaza kuwa, siku ya Ijumaa Julai 26 iliwakamata Walibya 95 baada ya kuvamia shamba ambalo linaonekana kutumika kama kambi ya kijeshi.
Donald Mdhluli, msemaji wa Polisi amesema kuwa, eneo hilo limeidhinishwa kama kambi ya mafunzo kwa kampuni ya ulinzi, lakini kwa mtazamo wa kwanza inaonekana kama kambi ya kijeshi.
Kwa mujibu wa polisi ya Afrika Kusini, Walibya 95 wanahojiwa kufuatia operesheni ya polisi iliyofanyika karibu na White River, katika jimbo la kaskazini mashariki la Mpumalanga, takriban kilomita 360 mashariki mwa Johannesburg.
"Mmiliki wa kampuni ya ulinzi ni raia wa Afrika Kusini," amesema Bw. Mdhluli, bila kutoa maelezo zaidi.
Picha za televisheni za operesheni hiyo zinaonyesha kuwepo kwa polisi wengi nje ya kambi inayoshukiwa, ambayo ilikuwa na hema za kijani zenye mtindo wa kijeshi na mifuko ya mchanga. Haijabainika mara moja iwapo Walibya waliokamatwa walikuwa na uhusiano na kundi lolote.
Tangu kuanguka kwa utawala wa Muammar Gaddafi mwaka 2011, Libya, nchi yenye utajiri wa mafuta, imekumbwa na ghasia na kugawanyika kati ya kambi mbili zinazohasimiana, huku magharibi kukiwa na serikali ya Abdelhamid Dbeibah, inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa, na serikali nyingine sambamba inayohusishwa na kambi ya Marshal Khalifa Haftar, kiongozi mwenye nguvu na mbababe wa kivita anayetawala mashariki na sehemu ya kusini.