Polisi: Watu 32 wauawa katika shambulio Somalia
Kwa akali watu 32 wameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya mshambuliaji wa kujitoa mhanga na watu wenye silaha kulenga eneo maarufu la ufukweni katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.
Hayo yanmeelezwa na Abdifatah Adan Hassan msemaji wa polisi ambaye ameeleza kuwa, watu 63 wamejeruhiwa katika tukio hilo huku hali ya baadhi yao ikiripotiwa kuwa mbaya.
Picha za video zilionyesha miili kadhaa na watu waliojeruhiwa katika wilaya ya Abdiaziz mjini Mogadishu.
Vyombo vya habari vya ndani vinasema kuwa, shambulio hilo lilitekelezwa na wanamgambo wa al-Shabab wanaodhibiti sehemu kubwa za kusini na katikati mwa Somalia.
Tangu mwaka 2007, magaidi wa al-Shabaab wamekuwa wakipigana na serikali ya Somalia na Kikosi cha Umoja wa Afrika nchini humo (ATMIS) lakini mashambulizi yake yamekuwa yakifeli hasa baada ya genge hilo kufurushwa kwenye miji mikubwa ya Somalia na kubakia katika baadhi ya vijiji ambako inavitumia kuendesha mashambulizi ya kuvizia na ya chini kwa chini.
Kikosi cha ATMIS cha Umoja wa Afrika kimetumwa huko Somalia kwa baraka kamili za Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.