UN yakaribisha hatua ya Juba kukubali kutumwa askari wa kikanda
Umoja wa Mataifa umepongeza hatua ya Sudan Kusini kukubali pendekezo la kutumwa askari wa kieneo nchini humo kufuatia mapigano ya ndani kati ya askari watiifu kwa Rais Salva Kiir na wafuasi wa aliyekuwa makamu wake, Riek Machar.
Ban Ki-moon, Katibu Mkuu wa umoja huo amezitaka pande husika katika mapigano mapya ya Sudan Kusini kutekeleza wajibu wao kwa kuheshimu makubaliano ya amani na kuwadhaminia usalama wananchi wa nchi hiyo.
Ijumaa iliyopita, jumuiya ya kikanda ya IGAD ilitangaza kuwa, serikali ya Juba imekubali pendekezo la kutumwa askari wa nchi kadhaa za Kiafrika nchini humo.
Suala la kutumwa askari wa nchi kadhaa za Afrika nchini Sudan Kusini ni miongoni mwa matakwa yaliyotolewa na Riek Machar ambaye aliukimbia mji wa Juba baada ya kushadidi mapigano. Mahboub Maalim, Mkurugenzi Mkuu wa Jumuiya ya Ushirikiano wa Kieneo ya Mashariki mwa Afrika IGAD alisema baada ya mkutano wa dharura wa wakuu wa jumuiya hiyo mjini Addis Ababa nchini Ethiopia kuwa, mbali na kutumwa askari wa kikanda nchini humo, Taban Deng Gai amekubali kujiuzulu wadhifa wake wa Makamu wa Kwanza wa Rais mara tu Riek Machar atakaporejea mjini humo.
Makubaliano ya kutuma askari wa nchi za Mashariki mwa Afrika nchini Sudan Kusini yamefikiwa baada ya mapigano makali ya hivi karibuni katika mji mkuu wa nchi hiyo Juba, ambayo yamesababisha vifo vya watu zaidi ya 300 na kujeruhi maelfu ya wengine mbali na kulazimisha makumi ya maelfu ya wengine kuwa wakimbizi.