DRC yajipanga kwa sensa ya kwanza ya kitaifa baada ya miaka 42
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i140544-drc_yajipanga_kwa_sensa_ya_kwanza_ya_kitaifa_baada_ya_miaka_42
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) inajiandaa kufanya sensa yake ya kwanza ya kitaifa baada ya zaidi ya miongo minne, kazi kubwa inayolenga kuwapatia hadhi rasmi mamilioni ya raia ambao wameishi bila vitambulisho vya kitaifa vilivyotolewa na serikali.
(last modified 2026-08-10T03:15:34+00:00 )
Aug 10, 2026 03:12 UTC
  • Kongo kufanya sensa ya kwanza ya kitaifa
    Kongo kufanya sensa ya kwanza ya kitaifa

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) inajiandaa kufanya sensa yake ya kwanza ya kitaifa baada ya zaidi ya miongo minne, kazi kubwa inayolenga kuwapatia hadhi rasmi mamilioni ya raia ambao wameishi bila vitambulisho vya kitaifa vilivyotolewa na serikali.

Zoezi hilo, la kwanza tangu mwaka 1984 wakati nchi hiyo ilipokuwa ikijulikana kama Zaire, linakusudia kuchukua nafasi ya makadirio ya muda mrefu kwa takwimu halisi na zenye kuaminika ili kuboresha upangaji wa huduma za umma katika nchi hiyo pana sana.

Zoezi la kuhesabu watu nchini kote katika sensa hii ya kwanza baada ya miaka 42 limepangwa kufanyika mwezi Julai 2027. Hatua za maandalizi, uhamasishaji wa umma, na shughuli za uchoraji ramani wa kidijitali zitaendelea katika mwaka huu wa 2026.

Kwa raia wengi wa Congo, sensa hii ni zaidi ya zoezi la takwimu tu; ni hatua muhimu kuelekea kutambuliwa rasmi na serikali. Huko Bunia, mji mkuu wa mkoa wa Ituri, Heritier Ramazani, mwenye umri wa miaka 28, hajawahi kuhesabiwa katika sensa ya kitaifa na hana hati yoyote rasmi inayothibitisha uraia wake.

Ukosefu huu wa nyaraka ni tatizo linaloenea, lenye mizizi katika miaka mingi ya misukosuko ya kisiasa, mifumo dhaifu ya kiutawala, na migogoro ya mara kwa mara.

Upeo wa kazi hii ni mkubwa sana, ikihusisha zaidi ya kilomita za mraba milioni 2.3. Ili kuweza kuisimamia vyema, Ofisi Kuu ya Sensa inapanga kutumia zana za kidijitali badala ya fomu za karatasi za kawaida. Henri Marie Kazadi, mratibu wa kiufundi katika Taasisi ya Taifa ya Takwimu, alibainisha kuwa mchakato utaanza kwa zoezi la uchoraji ramani wa kidijitali ili kubaini na kuweka kwa ramani maeneo yote yanayokaliwa na watu.

Hata hivyo, hali ya ukosefu wa usalama katika maeneo ya mashariki ni kikwazo kikubwa.

Sensa hii inakuja katika wakati nyeti wa kisiasa wakati nchi hiyo ikielekea katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2028.

Zaidi ya siasa, wachambuzi wa maendeleo wanasisitiza kuwa takwimu sahihi ni muhimu kwa miundombinu na ugawaji wa rasilimali.

Mchakato wa sensa ulianza kwa hatua ya kuajiri wafanyakazi wa mashinani mwezi Juni ili kusaidia hatua za awali za uchoraji ramani na ukusanyaji wa data.