Jeshi la Algeria laanzisha operesheni kali za kuwatambua magaidi
Wizara ya Ulinzi nchini Algeria imetangaza habari ya kuanza operesheni za kijeshi kwa lengo la kuwatambua wanachama wa makundi ya kigaidi nchini.
Taarifa iliyotolewa na wizara hiyo imesema kuwa, kikosi maalumu cha kupambana na ugaidi kimefanikiwa kumtia mbaroni gaidi hatari kwa jina la Mohamed Saïd, alias Saad katika eneo la Chekfa, lililopo katika mkoa wa Jijel, kaskazini mwa nchi hiyo. Taarifa hiyo imeongeza kuwa, gaidi huyo ametiwa mbaroni baada ya kujisalimisha mwenyewe kwa maafisa usalama. Hii ni katika hali ambayo jeshi la Algeria limefanikiwa kugundua mabomu manne yaliyokuwa yametegwa katika mkoa wa Tizi Ouzou.
Kwa mujibu wa Wizara ya Ulinzi ya nchi hiyo, gaidi Mohamed Saïd, alias Saad alikutwa na aina kadhaa za silaha za kijeshi ambazo zilikuwa tayari kwa ajili ya kutekelezewa vitendo vya kigaidi. Licha ya kwamba kwa sasa hali ya usalama nchini Algeria ni tulivu, hata hivyo nchi hiyo inakabiliwa na tishio la makundi ya kigaidi ambayo mara kwa mara yamekuwa yakitekeleza hujuma hizo.