Nchi za Afrika zapinga kazi za mchunguzi wa UN kuhusu ushoga
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i18847-nchi_za_afrika_zapinga_kazi_za_mchunguzi_wa_un_kuhusu_ushoga
Nchi za Afrika zimeanzisha jitihada za kusimamisha kazi ya mchunguzi huru wa kwanza wa Umoja wa Mataifa aliyeteuliwa kusaidia kazi ya kuwalinda mashoga na wale waliobadilisha jinsia zao duniani kote kutokana na vurugu na ubaguzi.
(last modified 2026-02-21T22:51:18+00:00 )
Nov 05, 2016 04:49 UTC
  • Nchi za Afrika zapinga kazi za mchunguzi wa UN kuhusu ushoga

Nchi za Afrika zimeanzisha jitihada za kusimamisha kazi ya mchunguzi huru wa kwanza wa Umoja wa Mataifa aliyeteuliwa kusaidia kazi ya kuwalinda mashoga na wale waliobadilisha jinsia zao duniani kote kutokana na vurugu na ubaguzi.

Jana Ijumaa nchi za Kiafrika ziligawa muswada kwa wanachama wa kamati ya 3 ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa inayoshughulikia masuala ya haki za binadamu zikitaka kufanyika mashauriano kuhusu uhalali wa kuanzishwa cheo hicho na kuteuliwa Vitit Muntarbhorn kutoka Thailand, ambaye amepewa miaka mitatu ya kuchunguza unyanyasaji dhidi ya mashoga, wasagaji, huntha (watu wenye jinsia mbili ya kike na kiume) wale waliobadilisha jinsia zao na wanaojihusisha na maingiliano ya kujamiiana ya watu kadhaa.

Charles Thembani Ntwaagae

Mwakilishi wa Botswana katika Umoja wa Mataifa, Charles Thembani Ntwaagae ambaye alikuwa akizungumza kwa niaba ya nchi 54 za Afrika amesema nchi za bara hilo zinataka kusitishwa kazi za mchunguzi huo wa UN hadi pale utakapochukuliwa uamuzi kuhusu kadhia hiyo. Amesema masuala ya matamanio ya kingono na utambulisho wa kijinsia havipaswi kuhusishwa na taasisi za haki za binadamu.

Nchi nyingi za Afrika na Asia zinapinga suala la kuhalalishwa maingiliano ya kingono baina ya watu wenye jinsia moja zikisisitiza kuwa ni kinyume na maumbile, tamaduni za kijadi na mafundisho ya mbinguni.

Ban Ki-moon

Mwaka 2014 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon alisema kuwa jumuiya hiyo ya kimataifa itatambua rasmi ndoa za watu wenye jinsia moja baina ya maafisa na wafanyakazi wake. Suala hilo lilipingwa vikali na Russia ikisaidiwa na nchi kama Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Saudi Arabia, Misri, India, Pakistan, China na Syria.