Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ajiuzulu
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i19450-waziri_mkuu_wa_jamhuri_ya_kidemokrasia_ya_kongo_ajiuzulu
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Augustin Matata Ponyo amesema leo kuwa amejiuzulu wadhifa huo sambamba na mwafaka wa kisiasa uliofikiwa nchini humo ambao unamuongezea muda wa kubakia madarakani Rais Joseph Kabila.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Nov 14, 2016 11:39 UTC
  • Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ajiuzulu

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Augustin Matata Ponyo amesema leo kuwa amejiuzulu wadhifa huo sambamba na mwafaka wa kisiasa uliofikiwa nchini humo ambao unamuongezea muda wa kubakia madarakani Rais Joseph Kabila.

Kabila alipasa kuondoka madarakani tarehe 19 mwezi Disemba. Hata hivyo muungano unaotawala na baadhi ya makundi ya upinzani mwezi uliopita yaliafikiana kuchelewesha uchaguzi wa rais hadi mwezi Aprili mwaka 2018 na kusisitiza kuwa, sababu kuu ya kuakhirishwa uchaguzi huo ni matatizo ya kilojistiki katika kuwaandikisha wapiga kura na uhaba wa fedha.

Waziri Mkuu aliyejiuzulu wadhifa huo wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ameviambia vyombo vya habari kuwa, amekabidhi hati ya kujiuzulu kwa Rais sambamba na makubaliano ya kisiasa yaliyosainiwa tarehe 18 mwezi Oktoba mwaka huu. 

Mrengo mkuu wa upinzani nchini Kongo umepinga makubaliano hayo yalisainiwa kati ya serikali ya Kinshasa na baadhi ya makundi ya kisiasa. Itakumbukuwa kuwa watu zaidi ya 50 waliuawa mwezi Septemba mwaka huu hmjini Kinshasa katika ghasia na maandamano ya mitaani ya wananchi wakishinikiza kuondoka madarakani Rais Joseph Kabila.

Maandamano ya wapinzani Kinshasa mji mkuu wa Kongo DR