Marekani: Ni kweli tunao askari maalumu nchini Libya kwa ajili ya ujasusi
Marekani imekiri kuwa ina imetuma askari maalumu nchini Libya kwa ajili ya ujasusi na kukusanya habari za kiintelejensia.
Thomas Waldhauser, kamanda wa jeshi la Marekani barani Afrika, sambamba na kuthibitisha habari hiyo, amesema kuwa, lengo la kutumwa askari wa nchi yake huko Libya ni kukusanya ripoti za kiupelelezi na kushirikiana na serikali ya umoja wa kitaifa inayoongozwa na Fayez al-Sarraj, Waziri Mkuu wa Libya.
Waldhauser ameongeza kuwa, ikiwa itahitajika kuwepo ushirikiano baina ya Marekani na serikali ya umoja wa kitaifa nchini Libya katika kupambana na ugaidi wa genge la Daesh, basi askari hao wataendelea kuwepo muda mrefu zaidi nchini humo. Hii ni katika hali ambayo, Walibya wao wamekuwa wakisisitizia udharura wa kutatuliwa mgogoro wa nchi yao kwa njia za amani. Hata hivyo Marekani na madola ya Magharibi, ndio wahusika wakuu katika kuifanya hali ya mambo nchini humo kuwa mbaya zaidi.
Libya ilitumbukia katika dimbwi la machafuko, baada ya Muungano wa Kijeshi wa Nchi za Magharibi (NATO) kuingia nchini humo na kusaidia kuondolewa madarakani, Kanali Muammar Gaddafi, kiongozi wa zamani wa nchi hiyo mwaka 2011.