Kongo DR yatahadharisha ongezeko la wakimbizi wa Burundi nchini humo
Mkuu wa Kamisheni ya Taifa ya Kushughulikia wakimbizi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ametahadharisha juu ya ongezeko la wakimbizi wa Burundi kuzidi kiwango cha ukubwa wa kambi za kuhifadhi wakimbizi huko mashariki mwa nchi.
Christophe Migale ambaye ofisi yake ipo mji wa Uvira katika mkoa wa Kivu Kusini katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo amesema kuwa, hadi sasa karibu wakimbizi elfu 30 wa Burundi wapo katika kambi ya wakimbizi ya eneo la Fizi katika hali ambayo kambi hiyo ina uwezo wa kupokea wakimbizi elfu 20 pekee.
Christophe Migale amesema kuwa, akthari ya wakimbizi hao wamekuwa wakilala nje tangu miezi minne iliyopita kufuatia kujaa kambi hiyo ya wakimbizi eneo hilo huku wakiendelea kusubiria kuhamishwa kupelekwa sehemu nyingine.
Maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi Duniani yanayofanyika kila tarehe 20 ya mwezi Juni yalifanyika jana katika kambi ya eneo la Fizi nchini humo.
Shirika la Kuwahudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) limetangaza kuwa, watu milioni 65 na laki sita walikuwa wakimbizi kote duniani hadi kufikia mwishoni mwa mwaka uliopita wa 2016.