Mazungumzo ya kutatua mgogoro wa Libya yamalizika bila natija nchini Tunisia
Umoja wa Mataifa umemaliza mazungumzo ya kuutafutia ufumbuzi mgogoro wa Libya, yaliyokuwa yanafanyika nchini Tunisia, bila ya natija yoyote.
Shirika la habari la Reuters limeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, mazungumzoa ya kuondoa hitilafu baina ya makundi hasimu ya nchini Libya yaliyokuwa yanafanyika katika nchi jirani ya Tunisia, yalimalizika jana bila ya kupatikana maendeleo yoyote ya maana katika suala la kufanyika uchaguzi mkuu nchini Libya.
Umoja wa Mataifa ndio ulioitisha na kusimamia mazungumzo hayo baina ya timu ya Bunge la Mashariki mwa Libya na ile Bunge la Tobruk, lakini umeshindwa kuleta mwafaka baina ya makundi hayo.
Duru ya pili ya mazungumzo hayo ilianza hivi karibuni nchini Tunisia na imejadili makubaliano yaliyounda serikali ya umoja wa kitafa ya Libya yanayojulikana kwa jina maarufu la Makubaliano ya Skhirat.
Skhirat ni moja ya miji ya Morocco na Makubaliano ya Skhirat yalifikiwa mwaka 2015 chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa kati ya makundi hasimu ya Libya. Lengo la makubaliano hayo lilikuwa ni kumaliza mapigano ya ndani nchini Libya na yalipelekea kuundwa serikali ya umoja wa kitaifa inayoongozwa na Fayez al Sarraj.
Akitangaza kumalizika duru ya pili ya mazungumzo hayo, Ghassan Salame, mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Libya ametosheka na kusema tu kwamba mazungumzo hayo yanaendelea bila ya hata kusema yataendelea tena lini.
Mwaka 2011 nchi za Magharibi ziliingia kijeshi nchini Libya wakati wa kampeni ya kuupindua utawala wa Kanali Muammar Gaddafi na tangu wakati huo nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika haijawahi kupata utulivu hata mara moja.