Wahajiri wa Kiafrika wazidi kufa maji wakielekea Ulaya kutafuta maisha
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i36222-wahajiri_wa_kiafrika_wazidi_kufa_maji_wakielekea_ulaya_kutafuta_maisha
Kwa akali wahajiri watano wa Kiafrika wamefariki dunia baada ya boti yao kuzama katika bahari ya Mediterranean, magharibi mwa pwani ya Libya.
(last modified 2026-02-21T22:51:18+00:00 )
Nov 07, 2017 04:50 UTC
  • Wahajiri wa Kiafrika wazidi kufa maji wakielekea Ulaya kutafuta maisha

Kwa akali wahajiri watano wa Kiafrika wamefariki dunia baada ya boti yao kuzama katika bahari ya Mediterranean, magharibi mwa pwani ya Libya.

Habari zinasema kuwa, boti hiyo iliyozama jana jioni ilikuwa imebeba wahajiri 140. Inaarifiwa kuwa, baada ya ajali hiyo, aghalabu ya wahajiri hao walikataa kuokolewa na Gadi ya Pwani ya Libya na badala yake wakakimbilia meli ya mabaharia wa Ujerumani. 

Haya yanajiri siku chache baada ya miili mingine saba ya wahajiri haramu kupatikana ndani ya boti ya plastiki karibu na pwani ya Libya.

Wahajiri wa Kiafrika wakinusurika

Gadi ya Pwani ya Italia imesema miili hiyo ilipatikana jana, ambapo wahamiaji haramu wengine 900 waliokolewa, kusini mwa bahari ya Mediterranean, wakiwa ndani ya boti hafifu za plastiki wakielekea barani Ulaya.

Aidha  Ijumaa iliyopita, wahajiri 700 waliokolewa katika bahari ya Mediterranea. 

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Kimataifa la Uhamiaji, zaidi ya wahajiri haramu elfu 18 na 800 wametiwa mbaroni kuanzia mwanzoni mwa mwaka huu 2017 hadi kufikia tarehe 24 Oktoba katika maji ya Mediterranea, mbali na maelfu ya wengine kufa maji.