Maalim Seif amuonya Profesa Lipumba amtaka aache kukivuruga chama cha CUF Tanzania
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i42118-maalim_seif_amuonya_profesa_lipumba_amtaka_aache_kukivuruga_chama_cha_cuf_tanzania
Katibu Mkuu wa Chama Cha Wanachi (CUF), Maalif  Seif Sharif  Hamad, amemkemea mwenyekiti wa chama hicho anayetambuliwa na msajili wa vyama vya siasa nchini Tanzania, Profesa Ibrahimu Haruna Lipumba na kumtaka kuacha kukivuruga chama hicho.
(last modified 2026-01-14T08:12:18+00:00 )
Mar 24, 2018 12:15 UTC
  • Maalim Seif amuonya Profesa Lipumba amtaka aache kukivuruga chama cha CUF Tanzania

Katibu Mkuu wa Chama Cha Wanachi (CUF), Maalif  Seif Sharif  Hamad, amemkemea mwenyekiti wa chama hicho anayetambuliwa na msajili wa vyama vya siasa nchini Tanzania, Profesa Ibrahimu Haruna Lipumba na kumtaka kuacha kukivuruga chama hicho.

Maalim Seif amesema kuwa, muda walionao kwa sasa Wanacuf ni kwa ajili ya kukijenga chama hicho. Maalim ameyasema hayo leo wakati wa mkutano wake na wanachama wa chama hicho uliofanyika katika Hoteli ya Korini iliyopo Tandale jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine amewataka wanachama wake kuwa wamoja na kutoyumbishwa na upande wa CUF ya Lipumba.

Profesa Lipumba, Mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na msajili wa vyama vya siasa Tanzania

Amesema kwamba, Lipumba ni mtu asiye mkweli, na kuongeza kuwa, yeye ndiye aliyempokea Edward Lowassa katika Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA, hata hivyo siku chache baadaye akageuka na kudai kuwa hakubaliani na maamuzi ya kumkaribisha katika umoja huo. Mkutano baina ya Katibu mkuu wa chama hicho na wanachama hao umefanyika kwa lengo la kujenga mshikamano na umoja ndani ya chama hicho ambacho bado kinaendelea kushuhudia hali ya mchafukoge kati ya Maalim Seif na Profesa Lipumba.

Profesa Lipumba na Maalim Seif walipokuwa wakishirikiana

Katika uwanja huo, hivi karibuni Profesa Lipumba alinukuliwa akisema kuwa, chama hicho kilimdekeza kwa kiasi kikubwa Katibu mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad. Kwa mujibu wa Lipumba hali hiyo imesababisha chama hicho kushindwa kupata viongozi watakaoingia katika Baraza la Wawakilishi Zanzibar sambamba na kutokuwepo kwake kwenye Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).