Makumi ya magaidi wa al-Shabaab wauawa eneo la Hiran, Somalia
Kwa akali wanachama 30 wa kundi la kigaidi na kitakfiri la al-Shabaab lenye mfungamano na mtandao wa al-Qaeda wameuawa katika operesheni kali iliyotekelezwa na Jeshi la Taifa la Somalia katika eneo la Hiran jana Jumanne.
Mohammad Nur Agajof, msemaji wa jeshi katika eneo hilo amesema magaidi hao waliuawa katika operesheni ya jana Jumanne katika miji ya Beledwein, Mahas na Mataban katika eneo la Hiran, katikati ya nchi hiyo ya Pembe ya Afrika.
Amesema mbali na kuangamiza makumi ya wanamgambo hao, askari wa Somalia wameteka Kamandi Kuu ya magaidi hao katika eneo hilo, sanjari na kupata silaha za kijeshi zilizokuwa mikononi mwa wapiganaji hao wa Kitakfiri.

Haya yanajiri siku chache baada ya wanachama wa al-Shabaab kutekeleza shambulizi la kigaidi na kuua kwa akali watu watano katika uwanja wa mpira wa miguu katika mji wa Pwani wa Barawa kusini mwa Somalia.
Kundi hilo lilianzisha hujuma zake nchini Somalia mwaka 2007 kwa lengo la kuiondoa madarakani serikali ya nchi hiyo linayoituhumu kuwa ni serikali ya kikafiri.