Ethiopia yatoa msamaha kwa kiongozi wa upinzani aliyehukumiwa kifo
Serikali ya Ethiopia leo imetoa msamaha kwa kiongozi wa upinzani wa nchi hiyo mwenye uraia wa Uingereza ambaye alikuwa amehukumiwa adhabu ya kifo, ikiwa ni hatua mpya ya mlolongo wa utoaji msamaha na kuwaachia huru wapinzani iliyochukuliwa na serikali hiyo baada ya miaka kadhaa ya machafuko yaliyoshuhudiwa nchini humo.
Andargachew Tsige alihukumiwa kifo mwaka 2009, bila mwenyewe kuwepo mahakamani, kwa kuhusika na harakati za kundi la upinzani la Ginbot 7 na kupelekea kutiwa nguvuni miaka mitano baadaye huko nchini Yemen na hatimaye kukabidhiwa kwa serikali ya Ethiopia.
Andargachew alikuwa katibu mkuu wa kundi hilo linalopinga serikali ya Ethiopia, ambalo lenyewe linajitambulisha kama harakati ya mageuzi lakini limetangazwa na Addis Ababa kama kundi la kigaidi.
Mwanasheria Mkuu wa serikali Berhanu Tsegaye ametangaza leo kuwa Andargachew amepewa msamaha "chini ya mazingira maalumu" pamoja na wafungwa wengine 575.
Tsegaye amewaeleza waandishi wa habari kuwa maamuzi hayo yamechukuliwa kwa "nia ya kupanua anga ya kisiasa".
Andargachew Tsige anatazamiwa kuachiliwa huru katika muda wa siku mbili zijazo.
Maelfu ya wafungwa, wakiwemo viongozi kadhaa waandamizi wa upinzani wameachiwa huru nchini Ethiopia tangu mwezi Januari mwaka huu. Watu hao walikuwa wakikabiliwa na mashtaka mbalimbali yakiwemo ya ugaidi au kuchochea kuipindua serikali.
Misamaha hiyo ni sehemu ya mageuzi yaliyoahidiwa kutekelezwa na serikali ya Waziri Mkuu mpya wa nchi hiyo Abiy Ahmed Ali.../