Rais wa Sudan Kusini kuendelea kubakia madarakani hadi 2021
Bunge la Sudan Kusini Alhamisi limepiga kura kurefusha muda wa rais Salva Kiir kubakia madarakani hadi mwaka 2021.
Spika wa Bunge la Sudan Kusini Anthony Lino Makana amesema bunge hilo lilipiga kura kurefusha muda wa kubakia madarakani kwa rais Salva Kiir kwa muda wa miaka mitatu zaidi na kusema hatua hiyo ni dharura ili kuzuia kuwepo pengo la madaraka nchini humo.
Sheria hiyo itamruhusu Kiir kubakia madarakani hadi mwaka 2021 hata wakati akiwa anajishughulisha na duru ya hivi karibuni kabisa ya majadiliano ya kimkoa ya amani pamoja na makamu wake wa zamani ambaye hivi sasa ni kiongozi wa waasi Riek Machar katika kumaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe vya miaka minne sasa.
Uchaguzi ulikuwa ufanyike mwaka huu, lakini mzozo umesababisha muda wa kufanyika uchaguzi huo kushindikana. Waziri wa sheria Paulino Wanawilla , ambaye aliwasilisha mswada huo, alisema utazuwia serikali kutangazwa kuwa si halali, wakati muda wake wa kuwapo madarakani utakapomalizika.
Makumi ya maelfu ya wananchi wameshauwa na karibu milioni nne wengine wamekuwa wakimbizi kutokana na mapigano yaliyozuka Sudan Kusini mwezi Disemba 2013 baada ya Rais Salva Kiir kumtuhumu makamu wake wakati huo Riek Machar kuwa alipanga njama za kumpindua.