Mshindi wa urais DRC, Tshisekedi, apata uungaji mkono wa AU, EU
Nchi za Umoja wa Afrika (AU) na Umoja wa Ulaya (EU) zimesema zimetilia maanani uamuzi wa Mahakama ya Kikatiba ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambayo imetangaza kutambua ushindi wa Felix Tshisekedi katika uchaguzi wa rais nchini humo.
Maafisa wa AU na EU wakizungumza na waandishi habari mjini Brussels Ubelgiji baada ya mkutano wao wa pamoja wamesema wamejadili matokeo ya uchaguzi wa DRC uliofanyika Disemba 30 na kwamba wamezingatia uamuzi wa mahakama ya nchi hiyo ambayo imeidhinisha ushindi wa Tshisekedi. Hata hivyo wakuu wa AU na EU hawakutangaza moja kwa moja hadharani kuwa wamemtambua rasmi Tshisekedi kama mshindi wa uchaguzi huo.
Tume ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (CENI) ilimtangaza Felix Tshisekedi wa chama cha upinzani cha UDPS kuwa mshindi wa uchaguzi wa urais.
Katika matokeo hayo CENI ilisema kuwa, Felix Tshisekedi aliibuka mshindi kwa kujipatia asilimia 38.57 ya kura, akiwatangulia wagombea Martin Fayulu wa Lamuka na Emmanuel Ramazani Shadary aliyewakilisha muungano wa chama tawala nchini humo. Hata hivyo, Martin Fayulu anadai kwamba, yeye ndiye aliyeibuka mshindi katika uchaguzi huo kwa kupata asilimia 61 ya kura.