Maandamano ya wananchi yamng'oa Bouteflika madarakani Algeria, kaimu wake atangazwa
Televisheni ya al Nahar ya Algeria imetangaza kuwa, Spika wa Bunge la nchi hiyo, Abdelkader Bensalah ameteuliwa kukaimu nafasi ya Rais Abdulaziz Bouteflika kwa muda wa siku 45. Bouteflika ameeng'olewa madarakani kwa nguvu nchini humo baada ya kushadidi maandamano ya wananchi ya kumtaka ajiuzulu.
Shirika rasmi la habari la Algeria limetangaza kuwa, mkuu wa jeshi la nchi hiyo, Ahmed Gaid Salah alitoa tamko jana Jumanne akitahimiza kutangazwa kuwa Bouteflika hana uwezo tena wa kuwa rais wa nchi hiyo kutokana na ugonjwa.
Taarifa hiyo ilisema kwamba, kutokana na hali ilivyo Algeria hivi sasa, hakuna njia nyingine isipokuwa kutekelezwa kifungu nambari 102 cha Katiba ya nchi hiyo yaani kutangazwa kuwa rais aliyeko madarakani hana uwezo wa kuendesha nchi.
Shirika rasmi la habari la Algeria limeongeza kuwa, muda wa siku 45 wa mtu anayekaimu nafasi ya Bouteflika unaweza kuongezwa.
Siku ya Jumamosi, vyama vya upinzani nchini Ageria viliitisha kikao cha pamoja na kutaka kung'olewa kwa nguvu madarakani Rais Bouteflika na kuundwe baraza la kusimamia kipindi cha mpito hadi uchaguzi wa rais utakapofanyika.
Vyama hivyo vya upinzani vililiomba jeshi la Algeria kuwa pamoja na wananchi katika utekelezaji wa matakwa yao hayo.
Bouteflika (82) amekuweko madarakani nchini Algeria tangu mwaka 1999 yaani miaka 20 iliyopita na mara zote alikuwa akigombea urais na kutangazwa mshindi katika vipindi vinne vya miaka mitano mitano vilivyopita.
Licha ya kwamba ni mgonjwa sana kiasi kuwa hawezi kutembea ila kwa msaada wa kigari cha wagonjwa, lakini tayari alishatangaza nia ya kugombea urais kwa kipindi kingine cha tano, lakini maandamano makubwa ya wananchi yamelazimisha ang'olewe madarakani kwa nguvu.