Moise Katumbi kurejea DRC baada ya kufutiwa mashitaka
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i53323-moise_katumbi_kurejea_drc_baada_ya_kufutiwa_mashitaka
Moise Katumbi, mwanasiasa wa upinzani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambaye kwa sasa yuko uhamishoni nchini Ubelgiji, anatazamiwa kurejea nyumbani katika kipindi cha wiki mbili zijazo, baada ya Waendesha Mashitaka wa Serikali kufuta uchunguzi wa shitaka la jinai dhidi yake.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 07, 2019 02:11 UTC
  • Moise Katumbi kurejea DRC baada ya kufutiwa mashitaka

Moise Katumbi, mwanasiasa wa upinzani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambaye kwa sasa yuko uhamishoni nchini Ubelgiji, anatazamiwa kurejea nyumbani katika kipindi cha wiki mbili zijazo, baada ya Waendesha Mashitaka wa Serikali kufuta uchunguzi wa shitaka la jinai dhidi yake.

Katumbi aliyasema hayo jana Jumatatu katika mahojiano na kanali ya televisheni ya France 24 na kubainisha kuwa, "Nitarejea Lubumbashi Mei 20, kuungana na watu wangu na kuzifariji familia ambazo zimekuwa zikinyanyaswa. Nilikuwa nje ya nchi wakati wao walikuwa wanafanyiwa ukatili."

Amesema moja ya malengo yake kurejea nchini DRC ni kuizundua jamii ya Wakongomani sambamba na kuanzisha harakati ya kuhakikisha kuwa Katiba haifanyiwi marekebisho na wabunge wanaogemea mrengo wa rais mstaafu  Joseph Kabila, ambao ndio wenye idadi kubwa bungeni. 

Katumbi ambaye alikuwa anakabiliwa na mashtaka ya kuajiri mamluki wa kigeni wakiwemo askari kadhaa wa Kimarekani waliostaafu kwa lengo la kuangusha utawala uliopita wa Kabila, mwezi uliopita wa Aprili, mahakama ya DRC ilimfutia kifungo cha miaka mitatu jela, kwa shitaka lililokuwa likimuandama la 'wizi wa jengo la kifahari'. 

Katumbi na wafuasi wake mjini Lubumbashi

Septemba mwaka jana, Ofisi ya Mashtaka ya Umma nchini humo ilimzuia Moise Katumbi kuwania urais na kutishia kuwa angelikamatwa iwapo angelitia mguu wake nchini DRC, akikabiliwa na tuhuma za kuhatarisha usalama wa taifa. Felix Tshisekedi alitangazwa mshindi wa uchaguzi huo wa urais wa Disemba mwaka jana 2018.

Meya huyo wa zamani wa Katanga alikimbilia uhamishoni mwezi Mei mwaka 2016 baada ya kuhitilafiana kisiasa na rais mstaafu Joseph Kabila.