Maandamano makubwa yafanyika Kano Nigeria ya kutaka kuachiliwa huru Sheikh Zakzaky
Mji wa Kano nchini Nigeria jana (Jumapili) ulishuhudia maandamano makubwa ya kushinikiza kuachiliwa huru Sheikh Ibrahim Zakzaky, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria anayeshikiliwa korokoroni kwa miaka kadhaa sasa.
Waandamanaji hao wa Kano ambao nimji wa pili kwa ukubwa nchini Nigeria huko magharibi mwa Afrika walisikika wakipiga nara za kutaka kuachiliwa huru Sheikh Ibrahim Zakzaky.
Aidha waandamanaji hao wamesisitiza kuwa, Sheikh Ibrahim Zakzaky anaendelea kushikiliwa kinyume cha sheria, hivyo vyombo vya usalama vinapaswa kutii amri ya mahakama na kumuachiliwa huru mwanaharakati huyom wa Kiislamu.
Sheikh Zakzaky na mkewe walitiwa mbaroni tarehe 13 Disemba 2015 katika Huseiniya ya Harakati ya Kiislamu huko Zaria kufuatia shambulio la jeshi la nchi hiyo lililoua shahidi mamia ya Waislamu wasio na hatia.
Mahakama Kuu ya Nigeria ilitoa amri ya kuachiliwa huru mara moja mwanachuoni huyo mwezi Disemba 2016 na kuliwajibisha jeshi la nchi hiyo kuilipa familia ya Sheikh Zakzaky fidia ya dola laki moja na 50 elfu.
Hata hivyo jeshi, serikali na vyombo vya dola vya Nigeria vimekataa kabisa kutekeleza amri hiyo ya mahakama na hadi hivi sasa mwanaharakati huyo wa Kiislamu anaendelea kushikiliwa korokoroni kinyume cha sheria.
Ripoti mbalimbali zinaonyesha kuwa, afya ya Sheikh Ibrahim Zakzaky ni mbaya na kwamba, amekuwa akikabiliwa na muamala mbaya na mateso hali ambayo imezidi kuzorotesha afya yake.