Ajali ya boti yaua watu 12 nchini DRC, 50 hawajulikani waliko
Watu wasiopungua 12 wamepoteza maisha kufuatia ajali ya boti huko katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Gavana wa jimbo la Kasai nchini DRC, Dieudonné Pieme amethibitisha kutokea ajali hiyo na kusema mbali na kusababisha vifo, watu wengine zaidi ya 50 hawajulikana walipo.
Pieme amesema watu wengine kumi wamenusurika kifo katika ajali hiyo iliyotokea Ijumaa katika Mto Lukenye
Ameongeza kuwa chanzo cha ajali hiyo ni idadi ya abiria kuzidi uwezo wa usafirishaji wa boti hiyo. Aghlabu ya abiria hao walitoka katika jimbo la Sankuru na boti hiyo ilipanga kuelekea mji mkuu wa Kinshasa.
Ikumbukwe kuwa mwezi Mei mwaka huu takriban watu 100 walipoteza maisha baada ya boti waliokuwa wakiabiri kuzama katika Ziwa Kivu nchini DRC. Ajali kama hizo zimekuwa zikitokea mara kwa mara katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.