Ubalozi wa Iran wakosoa msimamo wa Denmark kuhusu kuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu
TEHRAN (IQNA) – Ubalozi wa Iran nchini Denmark umelaani vikali vitendo vya mara kwa mara vya kuvunjia heshima Qur'ani Tukufu ndani ya taifa hilo la Nordic.
Ubalozi huo umeelezea wasiwasi wake mkubwa kuvusu vitendo hivyo na kubainisha kushangazwa kwake na ukosefu wa hatua madhubuti kutoka kwa Copenhagen katika kukabiliana na vitendo hivvyo vya kuvunjia heshima Qur'ani Tukufu.
Taarifa hiyo ya kidiplomasia iliyotolewa Jumapili, inakuja kufuatia msururu wa matukio ambapo vitendo vya kuvunjia heshima Qur'ani Tukufu vimetokea nchini Denmark, kufuatia kuidhinishwa na mamlaka husika katika wiki za hivi karibuni.
"Ubalozi umeshangazwa sana na hali ya wazi ya mamlaka ya Denmark kukataa kuzuia uenezaji unaoendelea wa ghasia, unaodhihirishwa kwa maneno ya uchochezi na chuki dhidi ya wageni, pamoja na dharau kwa utakatifu wa Qur'ani Tukufu," taarifa hiyo imebaini.
Taarifa hiyo imesisitiza kuwa licha ya maombi ya Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC), yanayowakilisha mataifa 57 ya Kiislamu, Denmark imekataa kuchukua hatua madhubuti za kukomesha chuki inayoendelea kwa Waislamu duniani kote, kupitia kuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu.
Katika wito wa kuchukua hatua, ubalozi huo umesisitiza kushtushwa kwake kufuatia hujuma za kila siku dhidi ya Uislamu na Waislamu kote ulimwenguni. Ubalozi wa Iran mini Copenhagen umeitaka serikali ya Denmark kuchukua hatua zinazohitajika, kutekeleza majukumu yake ya kimataifa, ili kukabiliana na hali hii ya kutisha.
Zaidi ya hayo, ubalozi huo umeitaka Denmark kuzuia vitendo vya kuendelea kudhalilishwa Qur'ani Tukufu, na kushutumu vitendo vinavyoendelea kuwa ni "onyesho la ajabu" lililofichwa chini ya kivuli cha kulinda uhuru wa kujieleza.
Katika tukio la hivi karibuni, mwanamke, anayeaminika kuwa na asili ya Iran, aliripotiwa kufanya kitendo cha kuvunjia heshima Qur'ani Tukufu nje ya ubalozi wa Iran mjini Copenhagen siku ya Jumapili.
Katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita, watu wenye itikadi kali wamevunjia heshima nakala za Qur'ani Tukufu nchini Uswidi na Denmark. Katika hali ya kutatanisha, serikali za nchi hizo zimetetea vitendo hivyo kama matamshi ya "uhuru wa kujieleza," na kuibua hasira ya dunia nzima kutoka kwa jamii ya Kiislamu. Msukosuko huu umesababisha mataifa kadhaa kuwaita au kuwafukuza mabalozi wa Uswidi na Denmark.
Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu imezitaka nchi wanachama wake kuchunguza hatua zinazofaa, ziwe za kisiasa au kiuchumi, dhidi ya nchi ambako vitendo hivyo vinatokea.
Zaidi ya hayo, OIC imehimiza mshikamano wa kimataifa katika kupinga majaribio hayo ya uchochezi dhidi ya matakufu ya Waislamu.