Waziri wa ulinzi wa Iran asema vita haitatokea katika eneo
Waziri wa ulinzi wa Iran amesema katika mjibizo aliotoa kuhusiana na mivutano iliyozuka kati ya Jamhuri ya Azerbaijan na Armenia kwamba vita havitatokea katika eneo.
Baada ya vita vya siku 44 vilivyozuka mwaka 2020 kati ya Armenia na Jamhuri ya Azerbaijan katika eneo la Nagorno-Karabakh, nchi hizo mbili zilitia saini makubaliano ya kusitisha mapigano kwa upatanishi wa Russia; na baada ya hapo sehemu kadhaa za eneo hilo zilikabidhiwa kwa Jamhuri ya Azerbaijan; lakini licha ya kusainiwa makubaliano ya kusitisha mapigano, uhusiano kati ya nchi hizo mbili unaendelea kutawaliwa na mivutano huku kila upande ukimtuhumu mwenzake kuwa anakiuka makubaliano ya usitishaji vita.
Kwa mujibu wa ripoti za vyombo vya habari na mitandao ya kijamii katika eneo, tokea Septemba 5 vikosi vya Jamhuri ya Azarbaijan vimekuwa vikihamisha vifaru na zana za kijeshi kutoka sehemu moja hadi nyingine.
Kwa mujibu wa IRNA, Brigedia Jenerali Mohammadreza Ashtiani, Waziri wa Ulinzi wa Iran, amewaambia waandishi wa habari kando ya kikao cha baraza la mawaziri kilichofanyika leo kuwa misimamo ya Iran iko wazi na hakuna mabadiliko yoyote ya kijiografia yatakayotokea katika eneo. Huku akiashiria ufuatiliaji unaofanywa kwa matukio yanayojiri katika eneo la Caucasus, Waziri wa Ulinzi wa Iran amesisitiza kuwa, uchunguzi uliofanywa kuhusiana na matukio yanayojiri unaonyesha kuwa hakuna tukio lisilo la kawaida litakalojiri.../