Iran yalaani vikali kudhalilishwa Qur'ani Tukufu nchini Uholanzi
Iran imelaani vikali kitendo cha kuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu mara kwa mara nchini Uholanzi, na kuitaka nchi hiyo ya Ulaya kuheshimu hisia za mabilioni ya Waislamu kote duniani.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran Nasser Kan'ani alisema Jumatano kwamba, "Serikali ya Uholanzi inatarajiwa kuelewa wajibu wake wa kuzuia matusi dhidi ya maadili na matakatifu ya kidini ya Waislamu zaidi ya bilioni mbili duniani."
Ameshauri Uholanzi kuzuia "kujirudia kwa vitendo hivyo vya kulaumiwa vinavyofanyika kwa jina la 'uhuru wa kujieleza.'
Matamshi hayo yamekuja siku chache baada ya Edwin Wagensveld, kinara wa tawi la Uholanzi la kundi linalopinga Uislamu la PEGIDA, kurarua nakala ya Qur'ani Tukufu mbele ya Balozi za Uturuki, Pakistani na Indonesia mjini The Hague sambamba na kuutukana Uislamu na Waislamu.
Kisha aliwashukuru polisi wa Uholanzi kwa kumpatia ulinzi wakati wa kutekeleza kitendo hicho cha kinyama.
Siku ya Jumatatu, Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) vile vile ililaani kitendo hicho cha kuvunjia heshima Qur'ani Tukufu, na kuzitaka mamlaka za Uholanzi kukomesha vitendo vya uchochezi na vya chuki dhidi ya Uislamu.
Miji kadhaa kote Uholanzi, Uswidi na Denmark imeshuhudia visa kama hivyo vya kuvunjia heshima nakala za Qur'ani Tukufu tangu mwanzoni mwa mwaka huu.
Vitendo hivyo vya chuki, ambavyo vyote vimefanyika kwa idhini ya serikali za nchi husika na huku ulinzi ukitolewa na vikosi vyao vya usalama, vimeibua hasira na maandamano katika ulimwengu wa Kiislamu.