Sep 03, 2024 03:08 UTC
  • Iran: Dunia haitasahau nafasi ya UK katika kuundwa utawala wa Kizayuni

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa, mataifa ya kieneo na dunia kwa ujumla hayatasahau mchango na nafasi ya Uingereza katika kuundwa utawala wa kibaguzi wa Israel katika kitovu cha ulimwengu wa Kiislamu.

Nasser Kan'ani alisema hayo jana katika ujumbe alioutoa kwa mnasaba wa kumbukumbu ya kuuawa shahidi Rais Ali Delvari. Delvari alikuwa shujaa wa kitaifa nchini Iran ambaye alipanga harakati za upinzani za wazalendo dhidi ya vikosi vya wakoloni wa Uingereza vilivyouvamia mji wa Busher, kusini mwa nchi mwaka 1915.

Katika ujumbe wake huo, Kan'ani amesema kuwa: Taifa kubwa la Iran lina historia pana na ya kujivunia ya kupambana na tawala za kikoloni ukiwemo ukoloni wa Uingereza; mapambano yaliyopelekea Iran kupata uhuru wake wa kisiasa.

Ameeleza bayana kuwa, tabia ya kihistoria ya kupenda vita, kuleta mgawanyiko na kuzusha changamoto na migogoro katika masuala muhimu ya kikanda, likiwemo suala la Palestina, ndiyo sura halisi ya sera ya ukoloni wa Uingereza katika eneo la Asia Magharibi.

Tangazo la Balfour la UK lililopelekea kuundwa utawala pandikizi wa Israel

Kan'ani amesisitiza kuwa, mataifa ya eneo na dunia hayatasahau jinsi watawala wa Uingereza walivyounda utawala wa kibaguzi wa Israel katika kitovu cha ulimwengu wa Kiislamu.

Amebainisha kuwa, kwa kuunga mkono utawala wa Kizayuni, Uingereza inashiriki katika mauaji ya halaiki, mauaji ya umati, mateso na kufurushwa Wapalestina kwenye makazi yao katika Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.

Tags