Amano: Iran imeheshimu kikamilifu makubaliano ya nyuklia
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Nyuklia (IAEA) ameeleza kuwa Iran imetekeleza ahadi zake zote katika makubaliano ya nyuklia kati yake na madola makuu duniani.
Yukia Amano amesema hayo alipohojiwa na gazeti la Kifaransa la Le Monde, na kusisitiza kuwa, Iran imetekeleza makubaliano ya nyuklia bila ya tatizo lolote kuanzia mwezi Januari mwaka huu hadi sasa. Amano ameongeza kuwa Iran inaendelea kutekeleza ahadi zake kwa jamii ya kimataifa. Kabla ya hapo, Mkurugenzi Mkuu wa IAEA alithibitisha katika ripoti tatu za wakala huo baada ya kufikiwa makubaliano ya nyuklia kuwa Iran imeheshimu kikamilifu makubaliano hayo.
Hii ni katika hali ambayo Marekani inaweka vizuzizi hivi na vile na kukwamisha kutekelezwa ahadi za nchi za Magharibi kwa visingizio mbalimbali licha ya kwamba Iran imeheshimu vilivyo makubaliano hayo. Tarehe 14 mwezi Julai mwaka jana Iran na kundi la 5+1 zilifikia mapatano muhimu ya nyuklia yanayojulikana kwa kifupi JCPOA ambayo yamethibitisha kuwa miradi ya nyuklia ya Iran ni yenye malengo ya amani kikamilifu.