Brigedia Jenerali Ashtari: Lengo kuu la magaidi ni kuingia Iran
Kamanda wa polisi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, lengo kuu la magaidi ni kuingia Iran kupitia njia mbalimbali na kwamba polisi humu nchini wanapaswa kuwa tayari kukabiliana na magaidi kwa kupokea taarifa za kiitelijensia katika maeneo ya mipakani.
Brigedia Jenerali Hussein Ashtari Mkuu wa Polisi ya Iran amesema hayo leo akiwa katika mji wa Kermanshah magharibi mwa Iran na kuongeza kuwa, kuwepo washauri wa Iran huko Iraq na Syria sambamba na kuangamizwa magaidi kufuatia jitihada za jeshi na wananchi wa nchi mbili hizo, kumewafanya magaidi wakae mbali na mipaka ya Iran.
Brigedia Jerenali Ashtari amebainisha kuwa, maadui waliliweka katika ajenda yao ya kazi suala la kudhihirisha kivitendo chuki zao dhidi ya Iran, madhehebu ya Kishia na Uislamu kuwa ni tishio baada ya mwamko wa Kiislamu na kwamba Marekani,utawala wa Kizayuni na pia baadhi ya nchi za eneo la Mashariki ya Kati zilianzisha makundi ya kigaidi kwa jina la Uislamu baada ya kuanza harakati za Mwamko wa Kiislamu ili kukabiliana na wimbi hilo.
Brigedia Jenerali Ashtari ameongeza kuwa, Marekani ndiye muungaji mkono mkuu wa magaidi na kwamba muungano wa eti kupambana na Daesh unaoongozwa na Marekani mara kadhaa umekuwa ukivishambulia vituo vya kijeshi vya serikali ya Syria kwa maslahi ya Daesh na kulipatia silaha kundi hilo la kitakfiri. Mkuu wa Polisi ya Iran amesisitiza kuwa, mpango wa kulifanya eneo la Mashariki ya Kati kuwa la amani utaendelea sambamba na kushindwa hivi karibuni waungaji mkono wa magaidi hao huko Mosul Iraq. Amesema juhudi hizo zitaendelea kwa sababu fikra za kitakfiri na kigaidi bado zingalipo katika eneo hili.