Rais Rouhani: Waislamu wakabiliane na uamuzi wa Trump kuhusu Quds
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ametoa mapendekezo 8 kwa ulimwengu wa Kiislamu kwa ajili ya kukabiliana na uamuzi usio sahihi na kinyume cha sheria uliochukuliwa na Rais Donald Trump wa Marekani kuhusu Quds tukufu na kusema kuwa: Marekani inafuatilia maslahi ya Wazayuni na haiheshimu matakwa halali ya Wapalestina.
Dakta Hassan Rouhani ambaye alikuwa akihutubia kikao cha dharura cha viongozi wa nchi wanachama katika Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) mjini Istanbul huko Uturuki ameitaka jumuiya hiyo kulaani hatua ya Marekani ya kuutangaza mji wa Quds (Jerusalem) kuwa ni mji mkuu wa Israel na kuutaka Ulimwengu wa Kiislamu kuwa na umoja mbele ya utawala wa Kizayuni wa Israel, kwa sababu matatizo yote ya Umma wa Kiislamu yanaweza kutatuliwa kupitia njia ya mazungumzo.
Rais Rouhani amesema serikali ya Marekani inapaswa kuelewa vyema uhakika kwamba, Ulimwengu wa Kiislamu hautanyaza kimya kuhusu suala la hatima ya Palestina na kwamba kudharau maamuzi ya kimataifa na mitazamo ya karibu jamii yote ya kimataifa kuhusu kadhia ya Palestina hakutapita hivi hivi bila ya kulipa ghara kubwa ya kisiasa.
Katika pendekezo lake jingine, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amezitaka nchi za Kiislamu kuwa na msimamo mmoja wa kupinga uamuzi wa Marekani kuhusu Quds na kueleza msimamo huo kwa washirika wa Marekani hususan nchi za Ulaya.
Rais Rouhani amesisitiza pia udharura wa kutambuliwa tena suala la Palestina kuwa kadhia nambari moja ya Ulimwengu wa Kiislamu na kusema: Baada ya kushindwa kundi la kigaidi la Daesh huko Syria na Iraq na ulazima wa kudumishwa mapambano dhidi ya makundi mengine ya kigaidi, nchi za Kiislamu hazipaswi kughafilika na hatari ya utawala wa Kizayuni wa Israel na silaha za nyuklia za utawala huo ambazo ni tishio kwa dunia nzima.
Katika pendekezo lake jingine Dakta Rouhani amesema wawakilishi wa nchi za Kiislamu katika Umoja wa Mataifa wanapaswa kufuatilia daima nyendo na harakati za Israel na kuongeza kuwa: Umoja wa Mataifa hususan Baraza la Usalama na Baraza Kuu la Umoja huo zina nafasi muhimu sana katika kupinga uamuzi wa Marekani dhidi ya Quds.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu amesisitiza kuwa Tehran iko tayari kushirikiana na nchi za Kiislamu bila ya masharti yoyote kwa ajili ya kuitetea Quds tukufu na kusema adui mkubwa wa Wayahudi si Waislamu wala Waarabu bali ni mradi hatari sana wa Wazayuni.