Rais Rouhani: Iran imefanikiwa katika makabiliano na kudhibiti Corona
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, takwimu zinaonyesha kuwa Iran imefanikiwa pakubwa katika kukabiliana na ugonjwa wa Covid-19 ikilinganishwa na nchi nyingine za dunia.
Rais Rouhani ameyasema hayo leo katika sherehe ya kuzindua miradi ya kitaifa ya Wizara za Nishati na Kilimo katika mkoa wa Ilam kwa njia ya video na kuongeza kuwa, katika vita vya kupambana na virusi vya Corona vilivyoenea dunia yote Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inashikilia nafasi nzuri.
Kadhalika Rais Rouhani sambamba na kubainisha kwamba Iran imejitosheleza katika kudhamini mahitaji ya chakula na baadhi ya mahitaji muhimu, amesema kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imejitosheleza katika uzalishaji wa ngano, kiwango ambacho hapo kabla kilikuwa chini. Leo na kwa amri ya Rais Hassan Rouhani, kumezinduliwa na kutekelezwa miradi 123 ya maendeleo na uzalishaji ya Wizara ya Kilimo katika mkoa wa Ilam, magharibi mwa nchi.