Iran: Hakuna mpango wa kufanya mazungumzo yoyote na Marekani
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema, hakuna mpango wa kufanya mazungumzo yoyote na Marekani kwa sababu Washington haiwezi kuaminika kwa mazungumzo inayofanya.
Mohammad Javad Zarif ameyasema hayo leo katika mazungumzo na waandishi wa habari alipoulizwa kuhusu uwezekano wa kufanyika mazungumzo kati ya Tehran na Washington, ambapo amesema: Hakuna mpango wa kufanyika mazungumzo yoyote. Wamarekani wameonyesha kuwa hawawezi kuaminiwa kwa mazungumzo unayofanya nao wala matokeo ya mazungumzo hayo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameeleza kuwa, takribani dunia nzima imefikia hitimisho kwamba, makubaliano yoyote itakayofikia na Marekani, wakati wowote Washington itakapotaka itayapuuza makubaliano hayo; na akaongezea kwa kusema, badala ya serikali ya sasa ya Marekani kutafuta njia ya kuzusha visingizio irekebishe tabia na mwenendo wake.../