Spika Qalibaf: Mabeberu wana uadui uliopindukia dhidi ya Mtume Muhammad (saw)
-
Muhammad Baqir Qalibaf
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa hujuma na vitendo vya mabeberu vya kumvunjia heshima Mtume Muhammad (saw) ni kielelezo cha uadui uliokita mizizi wa mustakbirina dhidi ya ujumbe wa rehma na upendo wa Mtume huyo wa Mwenyezi Mungu.
Muhammad Baqir Qalibaf leo Jumamosi amejibu kitendo kiovu cha kuvunjiwa heshima Mtume Muhammad katika baadhi ya nchi za Ulaya kwa kuandika katika ukurasa wake wa Twitter kwamba: Hujuma ya kumvunjiwa heshima Mtume Muhammad (saw) imedhihirisha tena uhasama uliokita mizizi wa mabeberu dhidi ya ujumbe wa mtume huyo uliojaa upendo na rehma kwa ajili ya walimwengu wote.
Spika wa Bunge la Iran amesema Waislamu kote duniani watalaani kwa nguvu zote dhambi hiyo isiyosameheka na kubatilisha njama za maadui wa uadilifu na ubinadamu.
Jarida la Kifaransa la Charlie Hebdo Jumatano iliyopita, lilichapisha vibonzo vinavyomkebehi na kumvunjia heshima Mtume wa mwisho wa Mwenyezi, Muhammad (saw).
Kitendo hicho kiovu kimelaaniwa na Waislamu, wasomi, maulama na wanasiasa katika nchi mbalimbali za duniani.