Mar 21, 2021 16:57 UTC
  • Kiongozi Muadhamu: Marekani imekosea katika kuamiliana na Iran na pia inafanya makosa katika eneo

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuhusu kutoaminika Marekani katika masuala mbali mbali likiwemo suala la mapatano ya nyuklia ya JCPOA na kuongeza kuwa, Wamarekani wamekosea katika mauamala wao na Iran na pia wanakosea kwa ujumla katika masuala ya eneo la Asia Magharibi.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo leo kwa mnasaba wa siku kuu ya  Nowruz  yaani mwaka mpya wa Kiirani  ambao umeanza tarehe  Mosi Farvardin (Machi 21)  Mwaka1400 Hijria Shamsiya. Kiongozi Muadhamu amehutubu kwa  njia ya televisheni ikiwa ni katika kuzingatia kanuni za kiafya za corona. Ayatullah Khamenei ameanza kwa kulinganisha kuanza mwaka 1300 na mwaka huu mpya wa1400 na kusema: "Nukta moja ndogo ya kulinganisha na muhimu wakati wa kuingia nchi katika karne iliyopita iliyoanza mwaka 1300 ni hii kuwa,  tunaona kuwa mwaka 1300 ulianza kwa udikteta wa Reza Khan ambaye alipata madaraka kupitia mapinduzi yaliyotekelezwa na Uingereza. Nchi wakati huo ilitawaliwa na Reza Khan ambaye alikuwa tegemezi kwa Uingereza. Lakini sasa katika mwaka huu wa 1400 kutafanyika uchaguzi na hii ina maana ya utawala huru wenye kutegemea kura za wananchi."

Kiongozi Muadhamu ameashiria uchaguzi wa rais utakaofanyika Khordad 1400 au Juni 2021  na kusema uchaguzi ni sawa na ujenzi mpya wa nchi ambapo kwa njia hiyo serikali hupata pumzi mpya.

Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa, kwa mtazamo wa kigeni,  uchaguzi wenye ushiriki wa wananchi ni ishara ya nguvu za kitaifa na kuongeza kuwa, mashirika ya kijasusi ya baadhi ya nchi hasa Marekani na utawala wa Kizayuni, kwa muda sasa yamekuwa yakijaribu kuonyesha uchaguzi ujao kama ambao hautakuwa na ushiriki mkubwa na ili kufikia lengo lao hilo wanawatuhumu wanaoandaa uchaguzi kuwa tayari wameshaupanga wanavyotaka ili wananchi wapoteze motisha na wadhani kuwa kura zao hazina maana. Amesema maadui wanatumia mitandao ya kijamii kwa kiwango kikubwa ili kufikia lengo hilo.

Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria kadhia ya vikwazo na kusisitiza kuwa, mzingiro wa kiuchumi na vikwazo ni kati ya jinai kubwa  za serikali na kadhia hiyo haipaswi kutazamwa kwa jicho la kisiaasa na kidiplomasia.

Aidha amesema kuwa, kuliwekea taifa vikwazo kiasi kwamba haliwezi kununua dawa na vifaa vya tiba ni jinai na kwamba hii ni jinai ambayo inaweza tu kutendwa na nchi kama Marekani.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameendelea kusema vikwazo dhidi ya Iran ni jinai lakini pia kwamba vikwazo hivyo vimekuwa na manufaa kwani Iran imeweza kubadilisha tishio hilo kuwa fursa. Amesema vijana Wairani  wenye jitihada tele na hima wameweza kuhakikisha kuwa nchi haitegemei tena madola ya kigeni katika baadhi ya bidhaa.

Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Ayatullah Khamenei ameashiria sera za mashinikizo ya juu zaidi dhidi ya Iran ambazo zilitekelezwa na serikali iliyopita ya Marekani na ambazo zilifeli na kusema: "Iwapo serikali ya sasa ya Marekani inataka kuendeleza sera hizo za mashinikizo ya juu kabisa, basi nayo pia itafeli."

Ayatullah Khamenei amesema huyo mjinga aliyetangulia (Donald Trump) alitekeleza sera za mashinikizo ya juu akidhani kuwa Iran ingedhoofika na hivyo kuketi kwenye meza ya mazungumzo na hapo ailazimishe Iran dhaifu itii matakwa ya kiistikbari na ipoteze nguvu zake kwa fedheha lakini sasa kilichojiri ni kuwa ni Trump ndiye alifedheheka pamoja na nchi yake huku Iran ya Kiislamu ikiwa imesimama wima kwa nguvu na kwa heshima.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria mapatano ya nyuklia ya JCPOA na kusema, sera za Iran za kuamiliana na nchi zingine katika mapatano ya JCPOA na katika utekelezaji mapatano hayo zimetangazwa wazi na hivyo sera hizo za Tehran hazitabadilika. Aidha Ayatullah Khamenei ametangaza bayana kuwa, Marekani inapaswa kuondoa vikwazo vyote dhidi ya Iran na baada ya kubainika wazi kwamba vikwazo hivyo vimeondolewa, Iran itarejea bila tatizo lolote katika majukumu yake ya JCPOA. Aidha amesema Iran haiamini ahadi ambazo Marekani inatoa.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria madai ya baadhi ya maafisa wa Marekani kuhusu ulazima wa kuwepo mabadiliko katika JCPOA na masharti yake ili Marekani irejee katika mapatano hayo na kusema: "Naam, hali ya mambo na mazingira yamebadilika kuliko ilivyokuwa katika mwaka (wa Kiirani wa )1395 na 1396, lakini hayajabadilika kwa maslahi ya Marekani bali ni kwa maslahi yetu. Iran imekuwa na nguvu zaidi ikilinganishwa na mwaka 1395 (2015). Kwa hivyo iwapo JCPOA itabadilika inapaswa kuwa kwa maslahi ya Iran.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewahutubu Wamarekani na kusema: "Nyinyi mtatumbukia katika matatizo siku baada ya siku na hata hatima ya rais wa sasa haijulikani. Sisi hatuna haraka katika pendekezo hili. Kwani sisi nasi tunaamini kuwa fursa zinapaswa kutumiwa na hatutakuwa na haraka kwani baadhi ya wakati hatari huwa ni kubwa zaidi kuliko manufaa. Sisi tuliwaamini Wamarekani wakati wa Obama na tukachukua hatua kwa mujibu wa mapatano ya JCPOA lakini hawakutekeleza ahadi zao katika JCPOA. Waliondoa vikwazo katika makaratasi tu lakini wawekezaji, (waliotaka kuwekeza Iran) waliogopa (kutokana na vitisho vya Marekani). Kwa hivyo ahadi wanazotoa hazina thamani yoyote."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa, Wamarekani wamefanya makosa katika kuamiliana na Iran na pia katika masuala ya eneo wanafanya makosa. Ameongeza kuwa, uungaji mkono wa Marekani kwa utawala wa Kizayuni wa Israel ni kosa na pia ukaliaji wake mabavu ardhi ya Syria bila shaka ni kosa.

Aidha Kiongozi Muadhamu amesisitiza kuwa umma wa Kiislamu hautasahau na hautapuuza kadhia ya Palestina na kwamba hatua ya baadhi ya nchi kuanzisha uhusiano na Israel haina maana. Ameongeza kuwa, hujuma dhidi ya Yemen ilianza wakati wa utawala wa Wademocrat kabla ya Trump na hivyo Wamarekani ni wahusika katika jinai dhidi ya taifa la Yemen.

Tags