Rais wa Iran: Adui ameshindwa katika vita vya kisaikolojia dhidi ya Iran
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameashiria njama na vita vya kisaikolojia vya pande zote vya adui dhidi ya watu wa Iran na kusema: Pamoja na fitna zote hizo, leo taifa la Iran linajivunia kuwa adui ameshindwa.
Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyasema hayo Jumatano alipokuwa akihutubu katika kikao cha wazi cha Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu, Bunge la Iran, ambapo amewasilisha muswada wa bajeti wa mwaka 1402 Hijria Shamsia ambao unaanza Machi 21. Raisi ameongeza kuwa, pamoja na kuwepo fitna zote alizoanzisha adui katika uga wa vita vya kisaikolojia na kiuchumi sambamba na kuchochoea jamii ya kimataifa dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu lakini hii leo taifa kubwa la Iran linajivunia kuwa adui ameshindwa.
Kwingineko katika hotuba yake, Rais Raisi amesema, “Katika mwaka wa fedha wa 1401, serikali iliweza kupata mafanikio kwa ushirikiano wa watu wote wanaohusika". Rais ameongeza kuwa, "Sehemu ya kwanza ya muswada wa sheria ya bajeti ya 1402 ya nchi inayohusiana na makampuni ya serikali, iliwasilishwa kwenye Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu mwezi mmoja mapema kwa mujibu wa sheria, ili Bunge lipate muda zaidi wa kuipitia kwa makini.
Akibainisha misingi iliyotegemewa katika bajeti hiyo, Rais Raisi amesema "Jitihada zetu zote zililenga kuhakikisha kuwa bajeti hii inaenda sambamba na sera zilizoainishwa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu-Allah Amhifadhi- na hali kadhalika sera za Mpango wa Saba wa Maendeleo."