Rais wa Iran ampongeza Recep Tayyip Erdogan kwa kuchaguliwa tena kuongoza Uturuki
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ametuma pongeza kwa Rais Recep Tayyip Erdogan kwa kuchaguliwa tena kuongoza Uturuki na kusema kuwa, huo ni ushahidi kwamba wananchi wa nchi hiyo bado wanamwamini.
Sayyid Ebrahim Raisi amesema katika salamu zake hizo za pongezi kwamba ana imani kipindi chote kitakachofuatia cha urais wake kitaendelea kuwa na uhusiano wa kiudugu na kiurafiki na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Amesema, ana imani kwamba pande hizi mbili zitaendelea kutumia vizuri mifungamano yao ya kihistoria, kiutamadni, kidini, ujirani mwema na kuheshimiana kwa ajili ya kulinda manufaa ya mataifa haya mawili na kudumisha amani na utulivu na kuliletea ustawi na maendeleo eneo hili zima.
Jana Jumapili, wananchi wa Uturuki walishiriki katika awamu wa pili ya uchaguzi wa rais baada ya kukosekana mshindi aliyepata zaidi ya nusu ya kura kwenye awamu ya kwanza ya uchaguzi huo. Hadi wakati asilimia 96 za kura zilipokuwa zimeshahesabiwa, Erdogan alikuwa ameshapata asilimia 52.28 ya kura zilizompa ushindi ingawa matokeo rasmi hayajatangazwa.
Viongozi mbalimbali duniani akiwemo Rais Vladimir Putin wa Russia nao wameshatuma salamu za kumpongeza Erdogan kwa ushindi huo.
Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS, nayo imempongeza Erdogan kwa ushindi huo.