Iran yasema iko tayari kujiunga na kundi la "BRICS"
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Anayeshughulikia Diplmasia ya Uchumi amesisitiza kuwa Iran iko tayari kuwa mwanachama wa kundi la BRICS.
Kundi la BRICS linaundwa na nchi zinazoibukia kwa kasi kiuchumi duniani.
Mehdi Safari Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Anayeshughulikia Diplomasia ya Uchumi amesema kuhusiana na mchakato wa Iran kujiunga na kundi la BRICS kwamba: Nchi wanachama wa kundi la BRICS bado hazijaainisha vigezo vyao kwa ajili ya wanachama wapya na kwamba sasa ziko katika mchakato wa kuandika vigezo hivyo.
Safari ameongeza kusema kuwa: Ni rahisi Iran kwenda sambamba na vigezo vya kundi la BRICS kwa kuzingatia vigezo na uwezo wa nchi hii. Mehdi Safari amesema kuwa, hadi kufikia sasa nchi 19 zimeomba kuwa wanachama ndani ya kundi la BRICS, na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia ni kati ya nchi za mwanzo kutuma maombi kwa ajili ya kupatiwa uanachama katika kundi hilo.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameongeza kuwa: Tunaweza kufanya miamala yetu na Russia, Uchina, Brazil na Afrika Kusini kwa kutumia sarafu zetu za kitaifa badala ya dola.
Mehdi Safari amesisitiza kuwa, Afrika Kusini imemwalika Hossein Amir- Abdollahian Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran kushiriki katika mkutano wa kundi la BRICS, na kuhudhuria mkutano huo ni muhimu sana.