Ijumaa, tarehe 15 Mei, 2026
https://parstoday.ir/sw/news/uncategorised-i138380-ijumaa_tarehe_15_mei_2026
Leo ni Ijumaa tarehe 27 Dhilqaada 1447 Hijria sawa na tarehe 15 Mei mwaka 2026.
(last modified 2026-05-15T14:12:20+00:00 )
May 15, 2026 14:10 UTC
  • Ijumaa, tarehe 15 Mei, 2026

Leo ni Ijumaa tarehe 27 Dhilqaada 1447 Hijria sawa na tarehe 15 Mei mwaka 2026.

Tarehe 25 Ordibehesht ni siku ya kumbukumbu ya Abul-Qassim Firdowsi mwanafalsafa na malenga mashuhuri wa Iran.

Inasemekana kuwa Firdowsi alizaliwa mwaka 319 au 320 Hijria Shamsia katika mji wa Tus, kaskazini mashariki mwa Iran.

Miongoni mwa athari muhimu za malenga huyo wa Kiirani ni kitabu alichokipa jina la "Shahnameh". Kitabu hicho kilichosheheni historia ya jadi na utamaduni wa Iran kabla ya ujio wa Uislamu, kimefasiriwa kwa lugha mbalimbali.   *****

Tarehe 15 Mei miaka 250 iliyopita katika siku kama hii ya leo ilitengenezwa meli ya kwanza yenye kutumia mvuke.

Meli inayotumia nishati ya mvuke ilitengenezwa miaka 70 baada ya kuvumbuliwa nishati ya mvuke na mhandisi wa Kifaransa Denis Papin.

Utumiaji wa nishati ya mvuke katika meli ulileta mabadiliko makubwa katika sekta ya usafiri wa baharini.    ****

Miaka 167 iliyopita katika siku kama hii ya leo alizaliwa Pierre Curie msomi na mwanafizikia wa Ufaransa.

Kipaji cha masomo ya hesabati na fizikia alichokuwa nacho kilianza kuonekana tokea ujana wake, na hatimaye kuibuka kuwa mtafiti mkubwa katika nyanja hizo. Mwaka 1898 mwanafizikia huyo wa Kifaransa alifanikiwa kugundua Radium akisaidiana na mkewe Bi. Marie Pierre.

Pierre Curie aliaga dunia mwaka 1906.   ***

Siku kama ya leo tarehe 15 Mei 1919, Izmir moja kati ya miji ya kihistoria na muhimu nchini Uturuki, ulitekwa na wanajeshi wa Mustafa Kamal Pasha, mwasisi wa Jamhuri ya Uturuki, baada ya kujiri mapigano yaliyopelekea kuuawa watu wengi.

Mji wa Izmir uko magharibi mwa Uturuki, na harakati ya Warepublican ya Uturuki ilianziwa katika mji huo wa kihistoria.   ***

Miaka 86 iliyopita katika siku kama ya leo, yaani tarehe 15 Mei mwaka 1940, jeshi la Ujerumani liliivamia na kuikalia kwa mabavu nchi ya Uholanzi baada ya shambulio kubwa lililodumu kwa siku 5 katika Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

Wanajeshi wa Kinazi wa Ujerumani walianza kuzishambulia nchi za Ufaransa, Ubelgiji, Uholanzi na Luxemburg huko magharibi mwa Ujerumani tarehe 10 Mei na kufanikiwa kuzidhibiti nchi zote hizo. Uholanzi ilijipatia uhuru wake mwaka 1945.     ***

Siku kama ya leo miaka 33 iliyopita, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliitangaza Mei 15 kuwa Siku ya Kimataifa ya Familia.

Uamuzi huo ulichukuliwa kutokana na umuhimu wa familia na asasi hiyo tukufu ambayo inahesabiwa kuwa msingi mkuu wa jamii na lengo ni kuilinda familia na madhara ya nje na ya ndani na kuifanya iwe na mchango na nafasi bora zaidi.

Asasi ya familia ilikuweko tangu wakati wa kudhihiri mwanadamu na imeendelea kuwa nguzo kuu ya jamii. Mke na mume na watoto na wakati mwingine bibi na babu ni watu wanaounda familia.

Familia ni mahala tulivu kwa wenza, sehemu ya kulea na kukuza watoto na ni mazingira yenye amani kwa ajili ya wanafamilia kuwa na mawasiliano salama.  ****

Na katika siiku kama hii ya leo tarehe 27 Dhulqaada miaka 11 iliyopita winchi ilianguka katika sehemu ya mashariki ya Msikiti Mkuu wa Makka (Masjidul Haram), na kuua mahujaji kadhaa wa Nyumba ya Mwenyezi Mungu.

Katika tukio hilo, lililotokea Ijumaa, tarehe 27 Dhu al-Qa’dah (Septemba 11, 2015) saa 11:10 jioni kwa saa za Makka, winchi ilianguka katika uwanja wa Masjidul Haram, na kuua watu 107 na kujeruhi wengine 238. Waathiriwa wengi walikuwa mahujaji kutoka India, Pakistani, Indonesia na Iran.

Serikali ya Saudi Arabia ilitangaza kwamba upepo mkali na dhoruba ndizo zilizosababisha kuanguka kwa winchi hiyo. Tukio hili, pamoja na janga la Mina wakati wa Eid al-Adha mwaka huo huo, yalikuwa miongoni mwa matukio ya kusikitisha zaidi ya ibada ya Hijja.